RAIS John Magufuli ametembelea eneo la kumbukumbu ya mashujaa waliopigania ukombozi wa nchi ya Namibia, lililopo nje kidogo ya Jiji la Windhoek nchini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Kwa mujibu taarifa iliyotolewa leo tarehe 28 Mei 2019 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Ras – Ikulu, Gerson Msigwa, Rais Magufuli ameongozana na Rais wa Namibia, Hage Geingob kuweka shada la maua kwenye eneo hilo linafahamika kwa jina la ‘Heroes Acre’.
Taarifa ya Msigwa inaeleza kuwa, mashujaa hao baadhi yao walipata mafunzo ya kijeshi kwenye Kambi ya Kongwa nchini Tanzania, wengine walikuwa maafisa wa chama cha SWAPO waliokuwa na ofisi zao jijini Dar es Salaam.
Pia,katika ziara yake nchini Namibia, Rais Magufuli amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Mstaafu wa Pili wa Namibia, Hifikepunye Pohamba jijini Windhoek.
Aidha, taarifa ya Msigwa inaeleza kuwa, Rais Magufuli ametembelea kiwanda cha nyama cha Kampuni ya Meatco kilichopo jijini Windhoek, ambapo alipata maelezo kutoka kwa Kaimu Mtendaji Mkuu wa kiwanda hicho, Jannie Breytenbach kwamba kina uwezo wa kuchinja ng’ombe 630 kwa siku na kuajiri wafanyakazi 650.
“Rais Magufuli amesema Tanzania ni nchi ya pili kwa idadi kubwa ya mifugo Barani Afrika na ameikaribisha kampuni ya Meatco kuja kuwekeza nchini Tanzania,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Msigwa.
Baada ya kumaliza ziara yake nchini Namibia, Rais Magufuli anatarajia kufanya ziara ya kitaifa nchini Zimbabwe kufuatia mwaliko aliopewa na Rais wa Taifa hilo, Emmerson Mnangagwa.
Leave a comment