HATUA ya Albert Chalamila, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya kuchapa viboko wanafunzi 14 wa Shule ya Sekondari ya Kiwanja na kurudisha nyumbani wanafunzi 392, imepongezwa na Rais John Magufuli. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
“Nimempongeza sana mkuu wa mkoa, kwa hiyo wakuu wa mikoa fika mahali tandika viboko,” amesema Rais Magufuli.
Akizungumza leo tarehe 4 Oktoba 2019, katika ziara yake mkoani Songwe, Rais Magufuli amesema, ipo haja ya kufanya marekebisho kwenye sheria inayozuia adhabu hiyo kwa kuwa viboko vinafundisha.
Amewaambia wananchi waliokuwa kwenye mkutano wake kwamba, hata Ulaya adhabu ya viboko ipo “nafikiri kama kuna mahali tulikosea kwenye ile sheria,” amesema na kuongeza “inabidi ikafanyiwe marekebisho.”
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo baada ya Chalamila kuwatandika vijana hao jana tarehe 3 Oktoba 2019, kwa madai ya kuhusika kuchoma mabweni mawili ya shule hiyo tarehe 1 Oktoba 2019.
https://youtu.be/TYsxPsNEo3g
Pamoja na kurudishwa nyumbani wanafunzi hao, Chalamila amewataka wazazi wa watoto hao kulipa Sh. 200,000 kila mmoja na wale waliohusika katika kuchoma moto mabweni hao kulipa Sh. 500,000.
Rais Magufuli amesitiza kwamba wanafunzi hao pale wataporejea shuleni, wanapaswa kurudi na fedha hizo kama ilivyoagizwa na Chalamila. “Na wale wengine (watano) waliohusika kabisa, peleka jela.” Amesema huku akisisitiza si kwamba hana huruma.
Leave a comment