RAIS John Magufuli anatarajiwa kuhudhuria sherehe za kuapishwa kwa Rais Mteule wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa zinazotarajiwa kufanyika kesho tarehe 25 Mei 2019. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa tarehe 24 Mei 2019 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa, Rais Magufuli leo ameongozana na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk. Jakaya Kikwete kuelekea nchini Afrika Kusini kwa ajili ya kuhudhuria hafla hiyo.
Pia, katika safari hiyo Rais Magufuli ameambatana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Profesa Palamagamba Kabudi na Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula.
Aidha, taarifa ya Msigwa inaeleza kwamba baada ya Rais Magufuli kuhudhuria sherehe hiyo, anatarajia kufanya ziara rasmi ya kitaifa nchini Namibia ikiwemo kuzindua mtaa uliopewa jina la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
“Prof. Kabudi amesema baada ya kuhudhuria sherehe za kuapishwa kwa Rais Mteule Ramaphosa, Rais Magufuli atafanya ziara rasmi ya kitaifa nchini Namibia ambako pia atazindua mtaa ulipoewa jina la Baba wa Taifa, Hayati Julius Nyerere kwa kutambua mchango mkubwa alioutoa katika ukombozi wa taifa hilo,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Msigwa.
Leave a comment