RAIS John Magufuli ameiagiza Wizara ya Fedha na Mipango kuchunguza matumizi ya Sh. 15.3 bilioni zilizotolewa na serikali kwa ajili ya kugharamia matumizi ya Mamlaka ya Usafiri wa Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu jana tarehe 26 Julai 2019, Rais Magufuli ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wafanyakazi wa Kituo Kikuu cha TAZARA jijini Dar es Salaam.
Taarifa ya Msigwa inaeleza kuwa, fedha hizo zilitolewa katika mwaka wa fedha wa 2017/18 na 2018/19 kwa ajili ya matengenezo ya injini saba kwa ajili ya kuboresha usafirishaji wa mizigo na ununuzi wa mitambo mipya ya mgodi wa kokoto za ujenzi wa reli.
“Fedha hizo zilitolewa kwa ajili ya matengenezo ya injini saba ambazo zingewezesha kumudu kusafirisha tani 400,000 za mizigo, kugharamia ukarabati mkubwa na ununuzi wa mitambo mipya ya mgodi pamoja na kuboresha miundombinu ya reli katika stesheni ya Fuga,” Inaeleza taarifa ya Msigwa.
Aidha, taarifa hiyo imeeleza kwamba Rais Magufuli anatarajia kuzungumza na Edgar Lungu, Rais wa Zambia kwa ajili ya kuchukua hatua madhubuti za kuimarisha miundombinu pamoja na kununua injini n mabehewa ya treni.
Wakati huo huo, Rais Magufuli amewataka wafanyabiashara wa soko la Kigogo Fresh lililopo Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam kutotoa ushuru wa soko wa Sh. 500 hadi pale Manispaa ya Ilala itakapowajengea choo.
Rais Magufuli ametoa agizo hili baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wananchi waliodai kwamba Manispaa ya Ilala haijawafikishia huduma ya maji na choo.
Leave a comment