IKIWA imebaki miezi takribani minane kuingia kwenye uchaguzi mkuu, baadaye mwaka huu, hitajio la Tume Huru ya Uchaguzi linazidi kushika kasi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wakati Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema Taifa na wanaharakati wengine wakiieleza dunia madhara ya kutokuwa na Tume Huru ya Uchaguzi, James Mbatia ameungana nao kupiga yowe hilo.
Ni kutokana na wanasiasa hususani wapinzani na taasisi za kiharakati kueleza kutoridhishwa na namna Tume ya Uchagu ya sasa inavyowajibika.
James Mbatia, Mwenyekiti wa Chama cha NCCR Mageuzi, ameitaka serikali kuitisha kikao cha maridhiano na wadau wa uchaguzi, ili kujadili upatikanaji wa Tume Huru ya Uchaguzi.
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 13 Februari 2020 jijini Dar es Salaam, Mbatia amesema suala hilo halipaswi kuchukuliwa kama suala binafsi, bali litazamwe kama suala linalohusi maslahi ya taifa.
“Tumelifanya suala la ubinafsi, badala masilahi mapana ya taifa. Hili sio suala la vyama vya siasa ni uhai wa taifa sio kusema la vyama vya siasa. Ni nani anayekubali kuelezea kusema hii ni tume huru na si tume huru. Suala la uchaguzi si suala la siasa ni la taifa,” amesema Mbatia.
Mbatia ameeleza kuwa, maridhiano ni juu ya upatikanaji wa tume hiyo ni ushindi kwa taifa, na si kwa vyama vya siasa, au serikali iliyopo madarakani.
“Maridhiano ni ushindi wetu sote, ushindi ni nini? Tumeshirikiana kwa pamoja hatujashindana. Ni kiburi tu na udhaifu wetu kujiona wema. Tusiseme yetu badala ya yangu tume ni ya Watanzania wote, kwa uhai wa watanzania. Na hii ni rai kwa wote leo uko madarakani leo haupo. Mkapa alikwepo ametoka akatumia busara akasema hili suala kwa Afrika tume ziwe huru. Waliko madarakani waache ubinafsi wazungumze umoja wa kitaifa.”
Aidha, Mbatia amesema chama chake kitafanya kikao cha Halmashauri Kuu yake ya taifa tarehe 19 Februari 2020, ili kutafakari namna ya kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwezi Oktoba mwaka huu.
“Tunajua mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi tumebaki miezi 8 tuingie kwenye uchaguzi. NCCR mageuzi ni mwasisi wa mageuzi. Licha ya yaliyotokea nyuma yote. Jana tulifanya kikao cha kamati ya halmashauri ya taifa. Tukakubaliana tutashiriki kwenye ngazi zote uchaguzi. Urais ubunge na wawakilishi na udiwani,” amesema Mbatia na kuongeza :
“Wiki ijayo tarehe 19 tumeitisha kikao cha halmashauri kuu ya taifa, ili kujenga mikakati kutekeleza shughuli hii na kutoa ratiba namna ya kujiandaa kushiriki uchaguzi.”
Leave a comment