HATMA ya kiungo wa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Jonas Mkude juu ya tuhuma za kinidhamu zinazomkabili, itajulikana kesho Jumamosi tarehe 23 Januari 2021. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mkude alisimamishwa na uongozi wa Simba, tarehe 28 Desemba 2020 pamoja na mambo mengine “tuhuma za utovu wa nidhamu zinazomkabili.”
Leo Ijumaa tarehe 22 Januari 2021, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Klabu ya Simba, Barbara Gonzalez alikuwa anazungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, kuhusu michuano ya Simba Super CUP itakayoanza 27-31 Januari 2021.
Michuano hiyo, itahusisha timu tatu za Simba, Al Hilal ya Sudan na TP Mazembe ya Congo.
Mara baada ya kumaliza kutangaza michuano hiyo, moja ya swali lililoulizwa na waandishi wa habari ni suala la Mkude lilipofikia hasa baada ya yeye (Mkude) kuomba radhi.
Akijibu swali hilo, Barbara amesema “kesi ya Jonas, iko kwenye kamati ya nidhamu, kesho inakutana na Mkude na itatoa mapendekezo kwa menejimenti nini cha kufanya na baada ya hapo, menejimenti itaamua.”
Katika video aliyojirekodi na kusambaa mitandaoni akiomba msamaha, Mkude alisema “tumeumbwa kukosea lakini haimaanishi nitakosea tena.”
“Mimi ni mwanasimba mwenzenu na klabu hii ni sehemu ya maisha yangu, ninaamini wachezaji wenzangu, benchi la ufundi, viongozi, wanachama na mashabiki mtanielewa na mtanisamehe,” alisema Mkude
Leave a comment