Friday , 29 March 2024
Home Kitengo Maisha Afya Johnson & Johnson wasitisha majaribio chanjo ya VVU Barani Afrika
AfyaTangulizi

Johnson & Johnson wasitisha majaribio chanjo ya VVU Barani Afrika

Spread the love

 

KAMPUNI ya Johnson & Johnson kutoka nchini Marekani imesitisha majaribio ya chanjo ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) Barani Afrika baada ya chanjo hiyo kushindwa kuonesha matokeo mazuri. Anaripoti Gabriel Mushi, Dar es Salaam … (endelea).

Chanjo hiyo iliyoanza kutolewa mwaka 2017 kwa baadhi ya nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara ambazo ni Malawi, Msumbiji, Afrika Kusini, Zambia na Zimbabwe, ilitolewa kwa wasichana 2,600.

Aidha, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa tarehe 31 Agosti, 2021na kampuni ya Johnson & Johnson kupitia kwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati Tendaji na Ofisa Mkuu wa Sayansi wa kampuni hiyo, Dk. Paul Stoffels, amesema ni jambo la kusikitisha kwamba majaribio ya chanjo hiyo yameshindikana licha ya ugonjwa huo kuathiri zaidi ya watu milioni 38 duniani.

Amesema majaribio ya chanjo hiyo iliyopewa jina la Imbokodo au kisayansi HVTN 705/HPX2008 ulikuwa ni mpango wa ushirikiano kati ya kampuni ya Johnson&Johnson, Kampuni ya dawa kutoka Marekani – Bill & Melinda Gates Foundation na Serikali ya Afrika Kusini.

“Wanawake wasiopungua 2,600 wenye umri kati ya miaka 18 hadi 35 kutoka Malawi, Msumbiji, Zambia, Afrika Kusini na Zimbabwe, walishiriki katika jaribio hili.

“Licha ya kwamba na nusu yao walipokea sindano nyingi za chanjo hiyo ya majaribio, miaka miwili baada ya sindano ya kwanza, matokeo yalionekana hayafai… hata kama chanjo hiyo ilitumiwa vizuri, ufanisi wake ni wa asilimia 25 tu!,” amesema Dk. Stoffels.

Aidha, Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu Mtendaji wa Baraza la Utafiti wa Tiba nchini Afrika Kusini (SAMRC), Profesa Glenda Gray ambaye pia ni Mwenyekiti wa mpango huo wa chanjo ya Imbokodo, amesema janga la maambukizi ya VVU bado ni changamoto kubwa Afrika.

Dk. Paul Stoffels

“Asilimia kubwa ya vijana na wanawake kusini mwa Afrika ndio waathiriwa wakubwa wa ugonjwa huu, licha ya maendeleo makubwa yaliyopatikana katika matibabu na kinga ya VVU.

“Bado ni changamoto kubwa kiafya ukanda huu, hii inatutaka kutumia maarifa yatakayopatikana kutoka kwenye majaribio haya kuendeleza utafiti wa chanjo ya VVU duniani,” amesema.

Kufuatia majaribio ya chanjo hiyo kubuma, Johnson&Johnson imesema inaendelea awamu ya tatu ya mpango wa majaribio ya chanjo nyingine ya VVU kwa wanaume wanaojamiiana na wanaume wenzao katika ukanda wa Amerika ya Kusini.

Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu Mtendaji wa Baraza la Utafiti wa Tiba nchini Afrika Kusini (SAMRC), Profesa Glenda Gray

IMBOKODO NI NINI?

Imbokodo ni neno lililotoholewa kutoka katika lugha ya kabila la Zulu huko Afrika Kusini.

Imbokodo maana yake ni jiwe au mwamba. Neno hilo limetokana na nahau kutoka katika kabila hilo inayosema kwamba “Ukimpiga mwanamke, Umempiga mwamba”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

Habari za SiasaTangulizi

CAG aibua madudu halmashauri 10, TANESCO na MSD

Spread the loveRIPOTI ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali...

error: Content is protected !!