KATIBU mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John John Myika, “ameutema rasmi” ubunge wake, katika jimbo la Kibamba jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu….(endelea).
Mnyika ambaye amekuwa mbunge wa Kibamba ambayo ilikuwa sehemu ya jimbo la Ubungo, kwa miaka 10 mfululizo, hayumo katika orodha ya wanachama wa Chadema, waliopigiwa kura za maoni, kutaka kuteuliwa kugombea nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020.
Hakuna taarifa zozote zinazoeleza sababu za mwanasiasa huyo, kutokugombea tena nafasi yake hiyo.
MwanaHALISI Online limeshindwa kumpata Mnyika kuzungumzia kutogombea kwake kwani simu yake ya kiganjani imekuwa ikiita pasina kupokelewa.
Hata hivyo, baadhi ya washindani wake ndani ya Chadema wanasema, mbunge huyo ameamua kutokugombea nafasi yake hiyo, kwa kuhofia kushindwa katika uchaguzi mkuu.
Wakati baadhi wakidai hivyo, taarifa zinasema, hatua ya Mnyika kujiweka kando katika kinyang’anyiro hicho, imetokana na kubanwa na majukumu ya nafasi yake ya ukatibu mkuu.
Mnyika alichaguliwa kuwa katibu mkuu wa chama hicho Desemba mwaka 2019 akichukua nafasi ya Dk. Vicent Mashinji ambaye jina lake halikupendekezwa na Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa chama hicho ili kuidhinishwa na wajumbe wa Baraza Kuu la chama hicho.
Katika mkutano wa kura za maoni uliyofanyika leo Jumanne, tarehe 14 Juni 2020, Ernest Mgawe, mwenyekiti wa Chadema katika jimbo la Kibamba, alitangazwa mshindi.
Mgawe alipata kura 30, kati ya 71 zilizopigwa. Wengine waliofuata nyuma ya Mgawe, ni Nemes Tarimo aliyepata kura 22 na Humphrey Sambo, ambaye alikuwa diwani wa Mbezi, aliyeambulia kura 19.
Leave a comment