SPIKA wa Bunge, Job Ndugai amemuandikia barua Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Semistocles Kaijage ya kumfahamisha kuwa Jimbo la Serengeti Mkoani Mara kwa sasa liko wazi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 1 Oktoba 2018 kwa umma na Kitengo cha Habari Elimu kwa Umma na Mawasiliano Ofisi ya Bunge.
Sehemu ya taarifa hiyo ineleza kuwa, Spika Ndugai amemuandikia barua Jaji Kaijage baada ya kupokea barua kutoka kwa Mbunge wa Jimbo la Serengeti, Marwa Ryoba Chacha ya kujiuzulu nafasi ya ubunge na kujivua uanachama wa Chadema.
“Mheshimiwa Spika ameandika barua hiyo kwa mujibu wa Kifungu 37(3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi (Sura ya 343, iliyojadidiwa mwaka 2015) kinachoelekeza kwamba, pale ambapo Mbunge, atajiuzulu, atafariki au ataacha kazi ya ubunge kwa sababu nyingine yoyote tofauti na zilizoainishwa katika kifungu cha 113 cha Sheria hiyo.
Spika atamjulisha Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi na kutangaza kwenye Gazeti la Serikali kwamba kiti hicho cha Ubunge kiko wazi.Kufuatia barua hiyo ya Mheshimiwa Spika, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) inaweza kuendelea na mchakato wa kumpata Mbunge wa kujaza nafasi hiyo iliyowazi ya Jimbo la Serengeti,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo.
Leave a comment