RAIS Mstaafu Dk. Jakaya Kikwete amesema huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto ni suala ambalo lipo ndani ya moyo wake na ataendelea kutoa mchango kwa Serikali na wananchi kwa ujumla. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Dk. Kikwete ametoa kauli hiyo leo tarehe 24 Januari, 2023 alipotembelewa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Dk. Kikwete ameishukuru Serikali kupitia wizara ya afya kwa kuendelea kumuamini na kumtumia katika mchango wake wa kuboresha huduma katika sekta ya afya nchini.
Naye, Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi ametoa shukrani za dhati kwa Rais Mstaafu Dk. Kikwete kwa mchango wake katika sekta ya afya alipokuwa rais na baada ya kustaafu hususan katika eneo la afya ya msingi, rasilimali watu, mafunzo ya kibingwa, afya ya mama na mtoto, huduma za meno na uwekezaji mkubwa katika Hospitali ya JKCI, Mlonganzila, Benjamin Mkapa na Chuo kikuu cha CUHAS.
Aidha, amesema hadi sasa Rais huyo wa awamu ya nne anaendelea kutoa ushirikiano yeye binafsi na taasisi yake ya Jakaya Mrisho Kikwete Foundation kwa Wizara ya afya katika jitihada za kuboresha huduma za afya hususani huduma za uzazi, mama na mtoto na kuendelea kuwa Balozi wa jitihada za kuboresha sekta ya afya nchini.
Leave a comment