SERIKALI imesema kutokana na changamoto ya upungufu wa maji katika Hifadhi ya Mkomazi inaendelea kuchimba mabwawa sita ili kukidhi mahitaji, anaandika Dany Tibason.
Hayo yameelezwa leo bungeni na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Ramo Makani alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Same Mashariki, Naghenjwa Kaboyoka (Chadema) ,ambaye alitaka kujua lini serikali itatatua kero ya maji katika eneo la hifadhi ya Mkomazi.
“Je ni lini Serikali itatengeneza miundombinu ya maji katika hifadhi ya Mkomazi ili kuzuia wanyamapori kuzurura kwenye makazi ya wananchi wakitafuta maji na kuharibu mazao yao,”?alihoji Kaboyoka.
Akijibu swali hilo, Makani amesema kutokana na changamoto ya upungufu wa maji serikali inaendelea kuchimba mabwawa sita ili kukidhi mahitaji hayo.
Amesema Bwawa moja lilikamilika katika mwaka wa fedha 2016-2017 na mengine matano yatachimbwa katika mwaka huu wa fedha 2017-2018.
Aidha, Naibu Waziri huyo amesema katika mwaka wa fedha 2017-2018, kisima kirefu kitachimbwa kwa ajili ya kusukuma maji na kujaza mabwawa yanayokauka ili kukidhi mahitaji ya maji wakati wa kiangazi kikali.
Leave a comment