HALMASHAURI ya Jiji la Mwanza, imeanza ujenzi wa soko kubwa la kisasa ambalo lilikuwa kwenye mikakati ya muda mrefu ya ujenzi na sasa mpango huo umekamilika. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Imesema haitawafumbia macho wanasiasa na wananchi watakaodiriki kukwamisha mradi huo kabambe ambao ni mkombozi kwa wafanyabiashara wa Jiji hilo.
Kauli hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi wa Jiji la Mwanza, Kiomoni Kibamba, wakati wa kikao cha robo ya pili cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo.
Kibamba alisema ujenzi wa soko hilo la kisasa utagharimu kiasi cha Sh. 23 bilioni na unatarajiwa kuanza Julai mwaka huu na kukamilika kwa kipindi cha miaka miwili.
Alisema kuwa ujenzi wa soko hilo litasaidia kuondokana na changamoto zilizokuwepo za ukosefu wa soko kwa ajili ya wafanyabiashara wengi wa jiji hilo.
Alisema kuwa tayari kuna watu wanaotaka kukwamisha ujenzi huo, kutokana na eneo ambalo wanataka kuwapeleka wafanyabiashara wa soko kuu na Mwadeco, kuanzisha migogoro.
“Shule ya msingi Mbugani ni ya Bakwata (Baraza la Waislamu Tanzania) na pia ni mali yetu, huo mgogoro ni wao wenyewe wabaki nao na Kama upo mahakamani hautafahamu hilo ila mradi utaendelea kama kawaida.
“Shule ya msingi Mbugani ilikuwa ni mali yetu (Serikali) na sio ya wananchi kwa hiyo miradi yetu ya kimkakati itaendelea kama kawaida,” alisema Kibamba.
Alisema kuwa miradi ya kimkakati ambayo ni ujenzi wa soko hilo Jiji pamoja na stendi ya kisasa ya Nyegezi, kwamba jiji la Mwanza wameipata kwa shida hivyo itakula sahani moja na wale watakaokwamisha.
Meya wa Jiji la Mwanza, James Bwire alimewataka watumishi wa jiji hilo kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha jiji hilo linafikia malengo yake ya ukusanyaji wa mapato.
Bwire alisema kuwa endapo watumishi hao watafanya kazi yao ipasavyo, ujenzi wa mradi huo utakamilika kwa wakati hatua ambayo itasaidia kuongeza ukusanyaji wa mapato ya jiji.
Katika hatua nyingine, Bwire aliwahimizi watendaji wa kata na mitaa jijini humo kuhimiza suala la usafi wa mazingira katika maeneo yao ili jiji hilo liweze kurudi katika nafasi yake ya kwanza kwa majiji nchini kwa usafi.
Leave a comment