RAIS Samia Suluhu Hassan amezindua jengo la mama na mtoto katika Hospitali ya CCBRT ambalo lina uwezo wa kuhudumia wajawazito 12,000 kwa mwaka. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yameelezwa leo Jumanne tarehe 5 Julai na Afisa Mtendaji Mkuu wa CCBRT, Brenda Msangi , katika hafla ya uzinduzi wa jengo hilo.
Brenda amesema jengo hili lina vitanda 160 vya kulaza wakina mama na kati ya hivyo vitanda 50 vimeunganishwa na mfumo wa hewa tiba ya oksijeni huku vitanda 46 vikiwa ni kwaajili ya watoto wachanga.
“Jengo hili lina miundombinu ya kuweza kufanikisha huduma kwa wajawazito hadi 12,000 kwa mwaka.
Tumejipanga kushirikiana na Serikali pamoja na wadau wengine kuongeza wanufaika wa huduma hizo hatua kwa hatua kuanzia akina mama 2,500 na wataendelea kuongezeka kadiri tutakavyojipanga,” amesema Msangi.
Amesema jengo hilo limejengwa kwa makadirio ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam na kanda ya mashi=ariki inayoongezeka kwa kasi na hivyo kuhitaji huduma zaidi.
Amesema jengo limejengwa kwa kuzingatia uhitaji wa manaume katika afya ya uzazi.
Amesema katika utoaji wa huduma jengo hilo litahakikisha ulemavu unagunduliwa mara tu baada ya mama kujifungua, “mfano nyayo zilizopinda, mgongo wazi, ambapo unaweka mkazo kuwaanzishia watoto matibabu mapema iwezekanavyo na hivyo kuwaepusha ulemavu wa kudumu.”
Msangi amesema akina mama 85 wameshapatiwa huduma katika jengo hilo tangu kuanzishwa kwa huduma tarehe 3, Julai, 2022 hadi sasa.
Amesema kati ya hao wapo walemavu, wenye historia ya fistula na watoto wenye utindio ya ubongo unaotokana na uzazi kinzani.
Amesema pia kuna kitengo maalumu cha uangalizi wa wagonjwa mahututi, kitengo cha usafi wa majengo na vifaa.
Pia Brenda ameongeza kuwa jengo hilo limezingatia uwepo wa vyumba 15 vya kutibia wagonjwa wa nje ili kupunguza foleni na kuruhusu akina mama 15 kufanyiwa uchunguzi kwa wakati mmoja na kufanya jumla yao kwa siku iwe akina mama 300.
Amesema pia katika jengo hilo kuna vyumba vya kujifungulia nane ambavyo mama anayejifungua anaruhusiwa kuingia na msaidizi mmoja ambaye atamchagua kama vile mume, mama au dada.
Leave a comment