MWANDISHI wa habari mkongwe nchini Tanzania, Jenerali Ulimwengu, anewataka Watanzania wajiulize kama wana uhuru wa kweli. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ulimwengu ameuliza swali hilo leo Alhamisi, tarehe 9 Desemba 2021, akihutubia kwa njia ya mtandao kongamano la miaka 60 ya uhuru wa Tanzania Bara, lililoandaliwa na Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha) na kufanyika jijini Dar es Salaam.
Mchambuzi huyo wa masuala ya siasa amesema, wananchi wanapaswa kuangalia maeneo yapi ya uhuru huo haujafika, kwani ndiyo nyenzo ya maendeleo yao.
“Tuangalie uhuru tuliopata tuone kama umekamilika, je umekamilima kweli? Je uhuru umekamilika kuona maeneo gani tunadhani uhuru haujafika, tuyafungue yale maeneo na wale wananchi wapate haki zao kufanya mambo yao kwa uelewa zaidi huku wakishirikiana ili waweze kuleta maendeleo ya jamii yao na wajue hakuna mtu anayeweza kuleta maendeleo na wawaogope wanasiasa wanaoomba kura ili walete maendeleo,” amesema
“Maendeleo hayaletwi na mtu, maendeleo sio nyanya wala kitungu, huletwa na wananchi wenyewe wanaosaidia kuleta maendeleo kwa uelewa mkubwa zaidi kubadilishana mawazo na kuelekezana,” amesema Ulimwengu.
Mwandishi huyo wa habari mkongwe nchini, amesema uhuru huenda sambamaba na utoaji huduma muhimu kwa wananchi wake.
“Uhuru ni mtu apewe elimu bora, kinga zote anazohitaji hadi aweze kujitambua, akishirikianae na wenzake, apate uhuru dhidi ya watawala wagandamizaji, dhidi ya watawala wanaotumia nafasi zao kujitajirisha, wanaotumia vyombo vya dola kujinufaisha wenyewe huku wananchi wanashindwa kunufaika,” amesema Ulimwengu.
Ulimwengu amesema, uhuru wa nchi lazima uambatane na uhuru wa wananchi wenyewe.
“Vilevile tupate uhuru dhidi ya uonevu ukandamizaji na rushwa, uhuru dhidi ya uozo wowote unaoweza kuwekwa kutugandamiza, kunyima uwezo wa kufanya kazi zetu.”
“Uhuru sio wa nchi bali wa wananchi, ni jambo la kuchekesha kama tungesema tumepata uhuru wa nchi bila wa wananchi. Ili uwe uhuru wa kweli lazima uambatane na uhuru wa wananchi kufanya maamuzi yao wenyewe bila vikwazo visivyo sababu,” amesema
Leave a comment