MKUU wa Shirika la Ujasusi la Marekani, William Burns amefanya mkutano wa siri na mwanzilishi mwenza wa kikundi cha wanamgambo wa Taliban, Mullah Abdul Ghani Baradar huko jijini Kabul nchini Afghanistan. Anaripoti Gabriel Mushi … (endelea).
Kwa mujibu wa Jarida la Washington Post wawili hao walikutana tarehe 23 Agosti mwaka huu. Mkutano huo unatajwa kuwa mkubwa zaidi na wa hadhi ya juu katika utawala wa Rais Joe Biden wa Marekani tangu Taliban washike madaraka.
Utawala wa Biden umewaondoa maelfu ya raia wake na wanajeshi huko nchini Afghanistan ili kuwaepusha na madhara yanayoweza kutokea baada ya Taliban kumtimua aliyekuwa Rais wan chi hiyo, Ashraf Ghani.
Burns ni mmoja wa wanadiplomasia wenye uzoefu zaidi wa Rais Biden wakati Baradar ambaye aliongoza ofisi ya kisiasa ya Taliban huko Qatar, ni mmoja wa viongozi wakuu katika utawala ambao umechukua madaraka huko Kabul.
Aidha, Msemaji wa CIA amesita kudhibitisha mkutano wa viongozi hao na kueleza kuwa shirika hilo kamwe haliwezi kuzungumzia safari za mkurugenzi wake.
Jarida la Washington Post ambalo halikutaja vyanzo vyake kuhusu mkutano huo, pia halikueleza kwa kina kuhusu mazungumzo kati ya mwanzilishi mwenza wa Taliban na bosi wa CIA.
Hata hivyo, inaelezwa kuwa walijadili kuhusu kuchelewa kumalizika kwa zoezi la kuwasaifirisha raia wa Marekani waliopo huko Kabul.
Biden ameweka tarehe ya mwisho ya Agosti 31 kumaliza kusafirisha wanajeshi wake wa Marekani na Uingereza lakini ameacha dirisha la kuongeza muda wa kusafirisha raia hao.
Hata hivyo, Msemaji wa Taliban, Suhail Shaheen alionya kuwa kundi hilo halitakubali kuongezwa na kuita tarehe hiyo ya mwisho kuwa mstari mwekundu.
Leave a comment