JAJI Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mustapha Siyani amejitoa kusikiliza kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka ya kupanga njama za ugaidi inayomkabili kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini humo, cha Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ametangaza kujitoa leo Jumatano, tarehe 20 Oktoba 2021, dakika chache kupita tangu alipomaliza kutoa uamuzi wa mapingamizi mawili yaliyowekwa na upande wa utetezi kwenye kesi ndogo ndani ya kesi kubwa.
Mapingamizi hayo yalihusu maelezo ya onyo ya mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo Adam Kasekwa, yasitumike mahakamani hapo kama sehemu ya ushahidi wa jamhuri na maelezo hayo yalitolewa baada ya Kasekwa kuteswa.
Katika uamuzi wake, Jaji Kiongozi Siyani amesema, kulikuwa na sababu ya msingi ya kutolewa nje ya saa 4 kwa mujibu wa sheria na kuhusu kuteswa upande wa utetezi haujathibitisha hilo.
Siyani aliyekuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma, alianza kusikiliza kesi hiyo tarehe 10 Septemba 2021, baada ya aliyekuwa akiisikiliza Jaji Elinaza Luvanda kujitoa.
Jaji Luvanda alitangaza kujitoa tarehe 6 Septemba 2021, baada ya Mbowe akiwawakilisha washtakiwa wenzake, kuomba ajitoe kwani hawana imani kama atawatendea haki, ombi ambalo alilikubali naye akajitoa.
Kwa upande wa Siyani, amejitoa ikiwa ni takribani siku wiki mbili zimepita tangu Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, alipomteua kuwa Jaji Kiongozi, tarehe 8 Oktoba 2021.
Siyani aliteuliwa kuchukua nafasi ya Eliezer Feleshi ambaye yeye aliteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
Akitangaza kujitoa, Jaji Kiongozi Siyani amesema, kesi hiyo ikiwa itakwenda mfululizo itawachukuwa takribani miezi minne na kwa kuwa yeye kwa sasa ana majukumu, “nimeona nijitoe aje Jaji mwingine haraka iwezekanavyo.”
Baada ya kueleza hayo, Jaji Kiongozi Siyani ameahirisha kesi hiyo hadi Msajili wa Mahakama Kuu atakapompangia jaji mwingine na watuhumiwa wamerejeshwa rumande katika gereza la Ukonga.
Mbali na Mbowe, watuhumiwa wengine katika kesi hiyo ni, Adam Kasekwa, Halfan Hassan Bwire na Mohammed Abdillah Ling’wenya.
Leave a comment