WAZIRI Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Seleman Jaffo ametangaza msimu wa tatu wa kujifukiza nyungu, ili kukabiliana na ugonjwa wa homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona (Covid-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Tabora … (endelea).
Akizungumza katika ziara ya Rais John Magufuli mkoani Tabora, leo Jumamosi tarehe 30 Januari 2021, Jafo amesema msimu huo utaanza tarehe 1 hadi 7 Februari 2021.
Waziri huyo wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ametoa kauli hiyo wakati anazungumzia tahadhari iliyotolewa hivi karibuni na Rais Magufuli kwa Watanzania, dhidi ya maambukizi mapya ya virusi vya ugonjwa huo.
“Na umesema watu wajifukize sana na rais naomba nikuambie, Jumatatu tuna anza kampeni nyingine ya ‘one week season three’ (wiki moja ya msimu wa tatu), nyungu kama kawaida. Tunanza tarehe 1 hadi 7, kazi inaendelea, uchumi wetu lazima usimame,” amesema Jaffo.
Tarehe 27 Januari 2021, wakati akizindua shamba la miti la Silayo lililopo Butengo wilayani Chato Mkoa wa Geita, Rais Magufuli aliwaomba Watanzania kuwa makini na ugonjwa huo, ikiwemo chanjo zinazoletwa kutoka nje ya nchi.
Kufuatia tahadhari hiyo ya Rais Magufuli kwa Watanzania, Jafo amesema licha ya kwamba Watanzania wako salama, lakini wataendelea kumuomba Mungu ili awaepusha na janga hilo.
“Juzi ulipokuwa unatangaza Shamba la Silayo, nilikufurahia sana mheshimiwa rais, ambapo ulisema Watanzania tuko salama. Angalia umati wote tuko salama, hapa corona haina nafasi, tutaendelea kumuomba Mungu kama ulivyotuelekeza,” amesema Jafo.
Msimu wa kwanza wa upigaji nyungu ulitangazwa na Jaffo, Aprili 2020, ambapo aliwataka Watanzania wapige nyungu pasipo kuona aibu ili kujikinga na corona. Waziri huyo alitangaza msimu wa pili wa nyungu Mei 2020.
Leave a comment