WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Selemani Jafo ameziagiza halmashauri zote kuhimiza uvunaji wa maji ya mvua ikiwa ni sehemu ya utunzaji wa mazingira. Anaripoti Danson Kaijage- Dodoma… (endelea)
Jafo ametoa kauli hiyo jana tarehe 15 Novemba, 2021 jiji Dodoma wakati akitoa taarifa ya wizara hiyo kwa waandishi wa habari kuelekea miata 60 ya Uhuru wa Tanganyika (Tanzania Bara)
Amesema ili kupata maji ya kutosha, utunzaji wa mazingira pamoja upandaji wa miti ni jambo muhimu.
“Hivyo halmashauri zinahakikishe majengo yanayojengwa yawe na mfumo wa uvunaji wa maji ya mvua,” amesema.
Jafo amesema itakumbukwa kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais ilianzishwa baada ya Muungano wa Serikali ya Tanganyika na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tarehe 26 Aprili, 1964 ulioasisiwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume.
Amesema baada ya Muungano, Mwalimu Nyerere alikuwa Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Sheikh Abeid Amani Karume alikuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wakati Rashid Mfaume Kawawa alikuwa Makamu wa Pili wa Rais.
Amesema katika kipindi cha miaka 60 ya Uhuru mafanikio yamepatikana kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) ambayo ni chachu katika ustawi wa Taifa.
“Serikali inahakikisha kuwa nchi yetu inaendelea kuwa yenye umoja, amani na usalama na Muungano wetu unaendelea kulindwa, kudumishwa, kuendelezwa na kuimarishwa.
Akizungumzia kuhusu muungano, Jafo amesema kuna mambo 22 ya Muungano kama yalivyoainishwa katika nyongeza ya kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 yanatekelezwa na Wizara na Taasisi zenye dhamana ya kusimamia mambo hayo.
“Baadhi ya mambo hayo yanahusu Katiba, Bunge na Utawala Bora, Uchumi, Fedha na Biashara; Ulinzi na Usalama, Diplomasia na Ushirikiano wa Kimataifa,Usafiri na Usafirishaji, Utabiri wa Hali ya Hewa, na Elimu, Sayansi na Teknolojia.
“Katika kipindi cha miaka 60, Serikali zote mbili zimefanikiwa kusimamia utekelezaji wa mambo hayo kwa ufanisi mkubwa na mafanikio yanaonekana katika nayanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Akizungumzia mafanikio, Jafo amesema kumefanyika mageuzi makubwa ya kiuchumi, kisiasa na kiutawala kwa lengo la kufufua uchumi, kuimarisha utendaji kazi serikalini na kukuza demokrasia na utawala bora.
“Mwaka 1996, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilianzishwa kwa Sheria ya Mamlaka ya Mapato Tanzania, Sura Namba 399.
“Mamlaka hiyo ina Ofisi pande zote mbili za Muungano (Tanzania Bara na Zanzibar) hivyo kurahisisha ukusanyaji wa mapato katika maeneo hayo.
“Nchi imeimarisha miundombinu ya barabara, usafiri wa anga, usafiri wa majini na huduma za kijamii katika pande zote za Muungano na kuendelea kutumia maliasili vizuri kwa manufaa ya wananchi kuliko ilivyokuwa kabla ya Muungano.
“Mafanikio haya, bila shaka, ndiyo yaliwezesha Tanzania kutangazwa kuingia kundi la nchi za uchumi wa kati kutoka kundi la nchi maskini mwezi Julai, 2020,” amesema Jafo.
Leave a comment