SULEIMAN Jaffo, Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, amempa mwezi mmoja Mganga Mkuu wa Manispaa ya Morogoro kufanya marekebisho ya kasoro zote zilizopo kwenye hospitali yake, anaandika Christina Haule.
Jaffo alitoa kauli hiyo alipofanya ziara ya kushtukiza katika hospitali hiyo na kukuta uchakavu wa magodoro, neti na ukosefu wa mashuka ya kulalia.
Waziri huyo amemtaka Dk. Barakael Jonas, Mganga Mkuu wa Manispaa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, John Mgalula kufanya marekebisho hayo kabla yua Aprili 3, 2017.
Pia amewataka viongozi hao kueleza kiasi cha fedha zilizoingia katika awamu ya tatu ya mfuko wa Basket Fund, na kuagiza taarifa zote za ujio wa fedha hizo na matumizi yake ziwasilishwe kwa Mkuu wa wilaya ya Morogoro ili aweze kufanya ufuatiliaji wake.
Waziri Jaffo alipewa taarifa fupi ya maendeleo yanayoendelea kufanyika katika hospitali hiyo na Mganga Mkuu wa Mkoa Dk Frank Jacob, ikiwemo kuanza kwa matumizi ya Tele Medicine, inayounganisha taarifa za moja kwa moja kutoka hospitali ya Taifa ya Muhimbili, mikakati ya kubadilisha Xray ya mfumo wa kizamani.
Baada ya kupokea taarifa hiyo Jaffo alitaka kuoneshwa baadhi ya maeneo ikiwemo wadi ya wazazi na majeruhi, ambapo alishuhudia wazazi waliojifungua kwa njia ya upasuaji wakiwa wametandika kanga kwenye vitanda vya hospitali huku wenye mashuka wakiwa ni wachache, huku magodoro na mashuka yakionekana chakavu.
“Lengo la ziara yangu ni kuona hali halisi ya hospitali ilivyo na kweli nimejionea. Tatizo mkipewa taarifa mnajiandaa kutandika mashuka wakati uhalisia huwa kunakuwa hivi.
“Inawezekana mashika yapo lakini angalia mama aliyejifungua kwa operesheni yeye na mtoto wake wanalala chini, hili haliwezekani linatakiwa kufanyiwa ufumbuzi haraka iwezekanavyo, amesema Naibu Waziri huyo.
Jaffo ameuagiza uongozi wa hospitali ya mkoa na ule wa wilaya, kutumia vyema fedha za mfuko wa Basket Fund, kwa ajili ya kuboresha huduma za afya, kwani theluthi ya fedha zote zinazotolewa kupitia mfuko huo, zimeelekezwa katika ununuzi wa vifaa tiba na dawa, na kwamba ni aibu kuona Serikali inaidhinisha bajeti na kutoa fedha kwa halmashauri za wilaya lakini bado muda wa bajeti umekuwa ukimalizika bila kufanyika kwa matumizi ya fedha hizo.
“Mwaka huu wa fedha serikali imeitengea Manispaa ya Morogoro Sh. 533 milioni za basket Fund, Morogoro Vijijini Sh. 923 milioni, kwa hiyo hizi halmashauri hizi mbili pekee zimepata Sh. 1.4 bilioni na theluthi moja inatakiwa kununua dawa na vifaa tiba,” amesema Jaffo.
Leave a comment