MAHAKAMA Kuu nchini Afrika Kusini, imetupilia mbali maombi ya dhamana ya aliyekuwa Rais wa Taifa hilo, Jacob Zuma, anayetumikia kifungo cha miezi 15 gerezani. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Mahakama hiyo imetupa maombi hayo leo Ijumaa, tarehe 9 Julai 2021, baada ya mawakili wa Zuma kuomba mteja wao aachiwe kwa dhamana, au apunguziwe adhabu.
Zuma aliyeanza kutumikia kifungo hicho tarehe 7 Julai 2021, alihukumiwa kutumikia adhabu hiyo, tarehe 29 Juni mwaka huu.
Baada ya Mahakama ya Kikatiba nchini humo kumtia hatiani katika kosa la kukaidi agizo lake, la kuhudhuria kwenye kesi ya ufisadi inayomkabili mhakamani hapo.
Baada ya Mahakama Kuu nchini Afrika Kusini kumnyima dhamana Zuma, mawakili wake wanatarajiwa kurudi katika Mahakama ya Kikatiba, Jumatatu ya tarehe 12 Julai 2021.
Siku hiyo majaji wa mahakama hiyo, wanatarajia kutoa uamuzi kama watamfutia au kumpunguzia adhabu Zuma.
Kwa mujibu wa mitandao ya kimataifa, Zuma huenda akapewa msamaha atakapotumikia adhabu hiyo katika kipindi cha miezi minne.
Awali Zuma aligoma kujisalimisha kwa mamlaka husika kwa ajili ya kuanza kutumikia adhabu hiyo, kwa maelezo kwamba kukaa gerezani kunaweza kumuathiri kiafya, kufuatia janga la Virusi vya Corona.
Zuma mwenye umri wa miaka 79, alipinga adhabu hiyo akihofia usalama wa maisha wake, akidai kwamba hali yake kiafya haiwezi kuhimili ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona.
Rais huyo mstaafu wa Afrika Kusini, anakabiliwa na mashtaka ya ufisadi na rushwa, wakati wa uongozi wake.
Zuma alikuwa Rais wa Afrika Kusini kuanzia 2009 hadi 2018.
Leave a comment