INSPEKTA Jenerali wa Polisi nchini Tanzania (IGP) Simon Sirro, amemshauri Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi, awashauri viongozi wa vyama vya siasa vinavyozuiwa kufanya mikutano, vikate rufaa kwa Waziri wa Mambo ya Ndani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
IGP Sirro ametoa ushauri huo leo Alhamisi, tarehe 23 Septemba 2021, baada ya kufanya mazungumzo na Jaji Mutungi, jijini Dodoma.
Kikao hicho kimehusisha maofisa waandamizi wa jeshi hilo ambacho ni maandalizi kuelekea kikao kati ya wadau wa siasa, asasi za kiraia na jeshi la polisi kitakachofanyika Dodoma 21 Oktoba 2021, Dodoma.
Mara baada ya kikao hicho, IGP Sirro amesema “tulichoona ni kwamba suala zima la kukata rufaa kwa waziri tunapokuwa OCD ametoa angalizo au amekataa kile kikao au mkutano usiendelee, basi ni vizuri akawashauri viongozi wa kisasa wakaona watumie ile forum ya kuweza kukata rufaa kwa waziri ili waziri aweze kubatilisha maamuzi ya OCD au kuona kama maamuzi ya OCD ni sahihi.”

Amesema mvutano baina ya jeshi hilo na wanasiasa kuhusu vikwazo vya mikutano yao ya ndani ni kutokuwepo kwa sheria rasmi inayoelekeza namna mikutano hiyo inafanyika.
“Kwenye suala zima la mikutano ya nje kwa kweli hakuna shida na si vyama vingi vinavyolalamika kwamba tumekuwa tunaingilia.”
“Lakini shida kubwa iko kwenye mikutano ya ndani na tumeona kwa upande wa sheria kwa kweli sheria ya Jeshi la Polisi lakini pia sheria ya vyama havijatamka bayana kuhusu sheria inanyotawala vikao vya ndani vya chama kwa hiyo tumeona kumekuwa na mwingiliano au sintofahamu,” amesema IGP Sirro.
Mkuu huyo wa jeshi la polisi amesema “kuna ombwe, kuna changamoto ya kutokuwa na sheria inayoelezea mikutano ya ndani maana yake ni nini.”
“Sheria inayotawala mikutano ya ndani ya namna gani, kwa hiyo tumemshauri msajili kwamba, hili ni vizuri wakalizungumza kama wanasiasa ili sisi tunaosimamia sheria tuweze kufika mahala tujue uelekeo ni nini,” amesema.

Hata hivyo, IGP Sirro amesema kuna wakati huzuia mikutano ya hadhara na ya ndani ya vyama vya siasa, kutokana na changamoto za kiusalama.
“Lakini jambo kubwa katika mikutano yote miwili, mikutano ya hadhara na ya ndani sisi jeshi tunaangalia usalama kwanza, tunaangalia suala la amani na utulivu.”
“Katika hiyo mikutano tukibaini amani na utulivu ni changamoto au kuna tishio lolote la amani na utulivu basi lazima tuchukue hatua kwa sababu ndiyo kazi yetu,” amesema IGO Sirro.
Leave a comment