INSPEKTA Jenerali wa Polisi (IGP) nchini Tanzania, Simon Sirro amesema, Polisi hawahusiki kutangaza mshindi wa Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020 bali kazi hiyo inafanywa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC). Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro … (endelea).
IGP Sirro ametoa kauli hiyo baada ya kuwapo kwa video inayozunguka mitandaoni ikionyesha Kamanda wa Polisi Wilaya ya Hai (OCD) Mkoa wa Kilimanjaro akimweleza Freeman Mbowe, mgombea ubunge wa Hai kwamba hatoshinda kwenye uchaguzi huo.
Katika video hiyo, inamwonyesha Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema akizungumza na OCD huyo aliyemwomba afanye mkutano huku OCD huyo akimtaka kuondoka akisema “panda kwenye gari uondoke, wewe utamshinda huyo, huwezi kumshinda hata ufanyaje, yaani kwenye mawazo yako (Mbowe) unawadanganya watu kwamba utamshinda, huwezi kumshinda hata ufanyaje.”

Kutokana na hilo, IGP Sirro amesema, timu kutoka makao makuu imekwenda kuchunguza hilo tukio kuona kuna nini, “suala la majibu kwamba utashinda au utashindwa siyo kazi polisi hata siku moja ni kazi ya tume.”
“Kwa hiyo tunachunguza kuona kuna jambo lina ukweli kutokana na ile ‘clip’ tutachukua hatua dhidi ya huyo ofisa. Niwahakikishe Watanzani kwamba tunachunguza,” amesema IGP Sirro
Amesema, jeshi la polisi lina taratibu zake ambazo askari wote wanapaswa kuzifuata “na polisi anakwenda tofauti na miongozi, tunamwajibusha kwa mujibu wa taratibu zetu.”
Leave a comment