INSPEKTA Jenarali wa Polisi Tanzania (IGP), Simon Sirro amewaomba wadau wa uchaguzi nchini humo kutimiza wajibu wao kikamilifu ili Uchaguzi Mkuu utakaofanyika kesho Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020 uwe wa amani. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Amewataja wadau hao ni; Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jeshi la Polisi na wanasiasa kuhakikisha kila mmoja kwenye nafasi yake kutimiza wajibu wao upasavyo na mshindi aliyechaguliwa na wananchi anatangazwa.
IGP Sirro amesema hayo leo Jumanne tarehe 27 Oktoba 2020 jijini Dar es Salaam, alipokuwa anazungumza na waandishi wa habari kuhusu maandalizi ya jeshi hilo kusimamia uchaguzi huo ambao kwa upande wa Zanzibar, kura zimeanza kupigwa leo.
“Mimi naamini, jeshi la polisi likitimiza wajibu wake, NEC wakatimiza wajibu wao, wanasiasa wote wakitimiza wajibu wao, mwisho wa siku tutapata viongozi kwa amani, vinginevyo tusipotimiza wajibu wetu, tutawaingiza Watanzania pabaya ambako hatukutarajia,” amesema IGP Sirro.
Katika kusisitiza hilo, IGP Sirro amesema, “niwatake tume ya uchaguzi kupitia wakurugenzi kupitia wasimamizi wa uchaguzi watimize wajibu wao, niwatake pia mawakala watimize wajibu wao, hao wadau wa uchaguzi mmoja wao katika uchaguzi asipotimiza wajibu wake matokeo yao ni fujo.”
Mkuu huyo wa jeshi la polisi ametoa onya kwa wanasiasa wanaohamasisha wafuasi wao kubaki vituo umbali wa mita 200 kwa ajili ya kulinda kura kutokufanya hivyo.
“Kumekuwa na msigano baadhi ya viongozi wa siasa wanahamasisha wapiga kura wakae na kulinda kura, ukikaa maana yake ni dalili ya kufanya fujo, wanaolinda kura kwa mujibu wa NEC ni mawakala ambao kila chama kimepeleka wakala wake anafanya kazi,” amesema IGP Sirro.
IGP Sirro amewaomba wagombea na wananchi kuwa tayari kupokea matokeo ya aina yoyote kwani katika ushindani kuna kushinda na kushindwa.
“Kuna baadhi ya vyama kama niliyosema wanaona wanashindwa kwa hiyo malengo na nia iliyopo ni kufanya fujo, niwaombe wanasiasa wakati huu si wakati wa kufanya fujo. Sisi Jeshi tutahakikisha kwamba tunatenda haki kuhakikisha yule atakayechaguliwa na wananchi anatangazwa,” amesema IGP Sirro.
“Rais mmoja, mbunge mmoja kwa kila jimbo, lakini nitoe onyo vikundi ambayo vimepanga kufanya fujo niwatake wasifanye uhalifu. Jambo la msingi kumbuka una familia yako inakutegemea na kama ni kijana mdogo huna familia yako una ndoto usijiingize kwenye matatizo yatakatisha ndoto zako,” ameonya IGP Sirro.
Leave a comment