TUNDU Lissu, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Bara, anawindwa na Jeshi la Polisi nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Simon Sirro, Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) akizungumza katika kipindi cha Dakika 45 kinachorushwa na Televisheni ya ITV amesema, jeshi hilo mpaka sasa halijamalizana na Lissu.
Na kwamba, Lissu hata akae miaka 20 Ulaya, atakaporudi nchini tu lazima ahojiwe kuhusu tukio lake la kushambuliwa.
Alisema, tangu ashambuliwe zaidi ya miaka miwili iliyopita, hawajapata ushirikiano wowote na kwamba yeye ni sehemu muhimu katika tukio lake la kushambuliwa.
Lissu aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki, alishambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana tarehe 7 Septemba 2017, mjini Dodoma. Kwa sasa ni mtia nia wa kugombea nafasi ya urais Chadema.
Amesema, si Lissu wala dereva wake aliyetoa ushirikiano “hata dereva wake tulipokwenda kumhoji, hakutaka kuonesha ushirikiano kwa Jeshi la Polisi.”
“Inakuwaje mtu ashuhudie tukio halafu polisi unashindwa kuwapa ushirikiano, hutaki hata kuwapa fursa ya kutaka wakuone, hapo sasa unategemea polisi watafanya nini?” amehoji.
IGP Sirro amesema, Lissu ni miongoni mwa watia nia wa urais katika chama chake (Chadema) kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 na kwamba iwapo atapata fursa hiyo, lazima arejee na hapo ndio watampata.
“Sasa ninashukuru kwamba kwa vile anagombea urais na kama atapewa nafasi na chama chake, ninafikiri atakuja nchini na tutamhoji vizuri tupate maelezo yake kwa sababu, upelelezi au tukio huwa halifiki mahala likawa mwisho,” amesema
“Hata kama angekaa Ulaya miaka 20, akija bado tutamhoji kujua ukweli wa jambo, lakini kwa vile anakuja, niombe aje, maana yake nina haja sana ya kutaka kuja kumhoji, ili kujua ukweli wa jambo lenyewe likoje,” alisema.
Baada ya tukio hilo la kushambuliwa mchana wa siku hiyo akitoka kuhudhuria mkutano wa Bunge, Lissu alipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Dodoma kwa matibabu ya awali na siku hiyohiyo usiku alihamishiwa Hospitali ya Nairobi nchini Kenya.
Lissu alipata matibabu Nairobi hadi tarehe 6 Januari 2018 alipohamishiwa nchini Ubelgiji kwa matibabu. Tayari mwanasiasa huyo maarufu ndani na nje ya Tanzania, amekwisha kueleza amemaliza matibabu na anachosubiri ni kurejea nchini mwake Tanzania.
Leave a comment