MKUU wa Jeshi la Polisi nchini (IJP), Simon Sirro, amefanya mabadiliko madogo kwa makamanda watatu wa mikoa wa polisi. Miongoni mwa waliobadilishwa, ni pamoja na Kamishena Msaidizi wa Polisi (ACP), Salum Rashid Hamdun. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kamishena Msaidizi Hamdun, alituhumiwa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola, kwa matumizi mabaya ya madaraka na uvunjifu wa taratibu.
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo Jumatano, tarehe 22 Januari na Mkuu wa Idara ya Uhusiano ya jeshi hilo na kusainiwa na Naibu Kamishena wa Polisi (DCP), Ahmed Msangi, imeeleza kuwa mabadiliko hayo yamefanyika ili kupisha uchunguzi juu ya madai ya waziri Lugola.
“Makamanda wote hao, wamehamishiwa makao makuu ya polisi ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizotolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola,” inaeleza taarifa hiyo kwa vyombo vya habari.
Wengine waliondolewa kwenye nyadhifa zao, ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACP), Ramadhani Ng’anzi, ambaye alikuwa kamanda wa polisi mkoa wa Arusha na aliyekuwa mkuu wa polisi wa mkoa wa Temeke, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Emmanuel Lukula.
Wiki iliyopita, Waziri Lugola, alitangaza kuwavua nyadhifa zao makamanda hao watatu. IGP Sirro aligoma kutekeleza agizo hilo mapema; kwa kuwa alikuwa anabanwa na taratibu za jeshi hilo.
Leave a comment