BENEDICT Ishabakaki, Mwanasheria wa Idris Sultan, mshindi wa Shindano la Big Brother 2014, amesema mchekeshaji huyo anatuhumiwa kwa kosa la kusambaza habari za uongo, na kujifanya rais. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Ishabakaki amesema hayo leo tarehe 1 Novemba 2019, baada ya mchekeshaji huyo kuhojiwa kwa mara ya pili, na Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, kuhusu tuhuma hizo zinazomkabili.
Ishabakaki amesema Idris amehojiwa kwa muda wa nusu saa, na kutakiwa kuripoti tena, siku ya Jumatano, tarehe 6 Novemba mwaka huu.
Vile vile, Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linashikilia simu zake, kwa ajili ya uchunguzi.
“Wamesema kosa lake la kwanza ni kusambaza habari za uongo, kinyume na kifungu cha 16 cha Sheria ya Makosa ya Mtandao. Kosa la pili ni kujifanya rais, kinyume na kifungu cha 15 cha makosa ya mtandao,” amesema Kashabakaki.
Idris amehojiwa kwa mara ya pili, baada ya jana kuhojiwa kwa muda wa saa tano. Baada ya kuhojiwa, mchekeshaji huyo alipekuliwa nyumbani kwake na maafisa wa polisi, kisha akaachwa huru kwa dhamana na kutakiwa kuripoti siku ya leo.
Idris aliripoti Polisi kuitikia wito wa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, aliyemtaka kujisalimisha polisi, kwa madai ya kwamba amevuka mipaka yake ya kazi.
Makonda alito agizo hilo, baada ya mchekeshaji huyo kuchapisha picha mbili katika ukurasa wake wa Twitter.
Picha ya kwanza iliyohaririwa inaonesha sura ya Rais John Magufuli, picha ya pili inaonesha Idris ameketi katika kiti cha Rais.
Leave a comment