KOCHA wa klabu ya As Vita Florent Ibenge amesema hawezi kuhofia wala kuogopa kucheza na Simba kutokana na ubora waliokuwa nao kwa sasa na wao wamekuja kucheza mpira. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea).
Mchezo huo wa kundi J, utapigwa kesho majira ya saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari kuelekea mchezo wa kesho Ibenge amesema kuwa wapo tayari kwa ajili ya Simba na wamekuja kucheza wala haogopi kucheza dhidi ya Simba bali anafurahi kucheza nao.
“Tunapenda mpira na tunapenda kuucheza, tumefanya kazi kubwa kuja kucheza dhidi ya Simba ambayo ni timu bora kwa sasa Afrika.
“Siogopi kucheza dhidi ya Simba ila nafurahia kucheza nao na tunataka kufurahia mchezo. Tukipoteza kesho tumetoka, kwa hiyo tumejipanga kuhakikisha tunapata matokeo”, amesema Ibenge.
Katika mchezo wa kwanza waliocheza nchini Jamhuri ya Congo, Simba iliibuka na ushindi wa bao 1-0.
Kwa upande wa mlinda mlango wa klabu hiyo Nathan, amesema wamekuja nchini Tanzania kwa aajili ya kucheza, walipoteza kwenye mchezo uliopita kutokana na kutocheza kama walivyotaka wao.
“Tulipoteza mchezo wa kwanza Kinshasa kwa sababu hatukucheza kama tulivyotaka, tumekuja Tanzania kwa ajili ya mechi ambayo tukishinda tutajiweka sehemu nzuri kwa ajili ya kufuzu hatua inayofuata.
“Mechi haitakuwa rahisi lakini kama Simba iliweza kushinda kwetu kwa nini sisi tushindwe kushinda kwao? Tutajitoa kwa ajili ya kupata ushindi”. Amesema kipa huyo.
Leave a comment