TANGU wachukue madaraka nchini Afghanistan tarehe 15, Agosti mwaka huu, viongozi kadhaa wa kundi la wanamgambo wa Taliban wameonekana hadharani mjini Kabul. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Hata hivyo, mmoja wao ambaye ni kiongozi wao mkuu wa kundi hilo, Haibatullah Akhundzada ameendelea kusalia mafichoni.
Jana tarehe 29 Agosti, 2021 wasemaji wa Taliban walisema kuwa Haibatullah Akhundzada yuko katika mji wa Kandahar.
“Amekuwa akiishi hapo tangu mwanzo,” amesema msemaji wa Taliban Zabihullah Mujahid wakati Naibu wake amesema kwa upande wake kwamba kiongozi huyo ataonekana hadharani hivi karibuni.
Haibatullah Akhundzada, mtaalam wa masuala ya kisheria na kidini, alitangazwa mwezi Mei 2016 kuwa kiongozi wa Taliban, kundi ambalo wakati huo lilikuwa limekubwa na malumbano ya ndani.
Aliteuliwa siku chache baada ya kifo cha mtangulizi wake, Mansour, aliyeuawa na shambulio la ndege isiyo na rubani ya Marekani huko Pakistan, kwa lengo kuu la kuunganisha tena Taliban.
Kundi hili liligawanyika kufuatia mapambano ya kuwania madaraka baada ya kifo cha Mansour na siri waliokuwa wameficha kwa miaka mingi kuhusiana na mwanzilishi wao, Mullah Omar.
Taliban ilitoa picha tu moja ya Haibatullah Akhundzada na hadi sasa hajawahi kuonekana hadharani.
Leave a comment