HUKUMU ya kesi ya madai ya kashfa iliyofunguliwa na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje katika Serikali ya Awamu ya Nne, Bernard Membe dhidi ya mwanahabari anayejitambulisha mwanaharakati huru, Cyprian Musiba imepigwa kalenda hadi Oktoba 28, 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Katika kesi hiyo namba 220 ya mwaka 2018, Membe amemshtaki Musiba, Mhariri wa gazeti la Tanzanite na Wachapishaji wa gazeti hilo ambapo anawadai Tsh. Bilioni 10 kwa kumchafua.
Hukumu ya kesi hiyo iliyokuwa itolewe leo Jumanne tarehe 12 Oktoba, 2021 na Jaji Joaquine De Mello imeahirishwa kwa sababu haijakamilika kuandikwa.
Wakili wa Membe, Jonathan Mndeme amesema hukumu hiyo imeahirishwa hadi Oktoba 28 kwa kuwa Jaji De Mello bado hajamaliza kuiandika.
Mbali na Musiba, wadaiwa wengine katika kesi hiyo ni Mhariri wa Gazeti la Tanzanite linalomilikiwa na Musiba na kampuni ya Tz Information and Media Consultant Ltd.
Musiba na wenzake katika kesi hiyo anashtakiwa kwa kumtuhumu Membe kuwa anamhujumu Rais John Magufuli asitekeleze majukumu yake ya kuwaletea wananchi maendeleo huku akidai kwamba mbinu mojawapo ya kukamilisha hujuma hizo ni maandalizi anayofanya kugombea urais mwaka 2020 kupitia CCM.
Bernard Membe alikuwa miongoni mwa wagombea Urais katika Uchaguzi Mkuu 2015.
Leave a comment