MAMLAKA ya Mkemia Mkuu wa Serikali imelenga kuimarisha utendaji kazi wa maabara katika kanda zake za Nyanda za juu kusini, na kanda ya ziwa kwa kuzipatia vifaa vya kisasa, anaandika Irene Emmanuel.
Akiongea na waandishi wa habari, Cletus Mnzava, Kaimu Meneja Masoko, Mawasiliano na Huduma kwa Wateja amesema lengo kuu katika kuimarisha shughuli za maabara ni kufanya uchunguzi maalum za kisayansi huko huko mikoani badala ya kuja Dar es Salaam.
Amesema wamejenga majengo ya kudumu ili kuwekeza vifaa vya kudumu tofauti na ilivyokuwa hapo awali.
“Ujenzi wa majengo hayo umeanza kwa baadhi ya kanda kama vile Nyanda za juu kusini amabapo jingo letu linatarajiwa kukamilika mwaka huu wa fedha, lipo eneo la Iwambi Mbeya, Arusha lipo Maeneo ya Mount Meru,” amesema Mnzava.
Miradi hiyo ya kuimarisha Maabara za Kanda inaendelea kutekelezwa kutokana na uelekezaji wa fedha zinazopatikana kwa ajili ya kuimarisha zaidi utoaji wa huduma za maabara kwa wananchi.
Mamlaka hiyo imevitaka vyombo vya habari kusaidia katika kufikisha ujumbe kwa wanajamii kuendelea kutumia huduma za Maabara ambazo zimesogezwa karibu zaidi na wanajamii katika Mikoa ya Mbeya, Katavi, Songwe, Rukwa, Lindi, Mtwara, Songea, Dar es Salaam, Pwani, Dodoma, Singida, Dodoma, Morogoro, Tabora, Iringa.
Leave a comment