HOSPITALI ya Rufaa ya Bugando (BMC), inakabiliwa na uhaba wa vifaa mbalimbali vya tiba pamoja na ugunduzi vikiwamo Xray na CT Scan hatua ambayo inachangia utoaji wa huduma usioridhisha, anaandika Moses Mseti.
Kauli hiyo imetolewa leo na Dk. Abel Makubi, Mkurugenzi Mkuu BMC mbele ya John Mongella, Mkuu wa mkoa wa Mwanza wakati wa uzinduzi rasmi wa jengo jipya, litakalokuwa linawahudumia wagonjwa wenye kadi za bima kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima Afya (NHIF).
Dk. Makubi amesema kwa zaidi ya miaka minne sasa hospitali hiyo inakabiliwa na ukosefu wa vifaa hivyo na kwamba tayari wameanza kuweka mipango na mikakati ya kununua baadhi ya vifaa ili kutoa huduma ambayo ni bora kwa wagonjwa wao.
Amesema baada ya kufika katika hospitali hiyo inayohudumia mikoa ya kanda ya ziwa na magharibi yenye watu zaidi ya milioni 14, amenunua mashine aina ya CT Scan ambayo ndani ya miezi miwili itakuwa imefika na kutoa huduma.
“CT scan sasa imenunuliwa na baada ya miezi miwili itakuwa tayari imefika, lengo ni kuhakikisha wagonjwa wetu wanaofika BMC wanapata huduma ambayo ni bora na kumaliza malalamiko ya muda mrefu yaliyokuwa yakitolewa na wananchi wetu.
“Pia zamani kulikuwepo na malalamiko kwa wananchi kwamba kuna lugha chafu zinazotolewa na wauguzi wetu kwa wagonjwa, lakini baada kufika hapa nimelimaliza suala hilo na sasa hivi hakuna tena kitu kama hicho,” amesema Dk. Makubi.
John Mongella, Mkuu wa mkoa huo, amesema kuimarishwa hospitali hiyo kutawasaidia wananchi wa kanda hiyo na hivyo kuacha kusafiri kwenda Dar es Salaam kufuata huduma.
“Asilimia 50 ya wagonjwa katika hospitali ya Ocean road na asilimia 60 ya wagonjwa wanaokwenda Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, wote wanatoka kanda ya ziwa ni lazima tuboreshe hospitali hii,” amesema Mongella.
Joseph Kasheku, Mbunge wa Geita Vijijini (CCM), amesema awali hospitali hiyo ilikuwa imeharibika kutokana na utoaji wa huduma mbovu ikiwemo na lugha mbaya aa wauguzi kwa wagonjwa jambo ambalo lilisababisha wananchi kuikimbia.
Leave a comment