WAKAZI wa Jiji la Dodoma wamehofia kupata magonjwa ya mlipuko wa matumbo au kipindupindu kutokana na kutozingatiwa kwa kanuni za usafi hususani katika soko la Sabasaba. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hofu hiyo imetanda kutokana na wafanyabiashara wa mbogamboga na matunda kuuza bidhaa zao katika mazingira hatarishi.
MwanaHALISI Online imeshuhudia wafanyabiashara wa mbogamboga na matunda wakiwa wanauza bidhaa hizo chini huku wakizungukwa na maji machafu ambayo yanaweza kusababisha magonjwa ya mlipuko.
Kutokana na hali hiyo baadhi ya wateja wamesema kuwa hali inaweza kusababisha magonjwa kutokana na wafanyabiashara hao kuuza mboga zao bila kufuata sheria na taratibi za kanuni za usafi.
“Zamani hapa sokoni Sabasaba kulikuwa na majaruba ya kulima mpunga kwa maana hiyo kulikuwa na maji mengi, lakini baada ya kubadilishwa matumizi na kuwa soko yalipungua.
“Hata hivyo kwa kipindi kama hiki cha mvua maji uvia na kuanza kutililika kila sehemu na mengine kufuata mkondo wake na hivyo yapo yanayotililika na mengine kutuama.
“Kwa maana hiyo hawa wafanyabiashara ya mboga ambao wanauza mboga zao kwa kuzitandika chini kwa maji haya machafu wanaweza kusababisha magonjwa ya mlipuko,” alisema mmoja wa wateja.
Kwa upande wake Afisa Afya wa Jiji la Dodoma, Abdallah Mahia, alipotafutwa kuzungumzia suala hilo alisema kuna changamoto kubwa kwa wafanyabiashara wa mbogamboga na matunda katika soko hilo.
Alisema wamekuwa wakitoa elimu mara kwa mara kwa kuwataka wafanyabiashara kufanya biashara zao kwa kuzingatia sheria na kanuni za afya ili kuweza kuepukana na magonjwa hatarishi.
“Ikumbukwe kuwa wale wanaofanyabiashara kwa kuzitandaza chini siyo wakudumu ndani ya soko hilo bali ni wakulima ambao wanaleta mboga zao kuja kuuza.
“Ila kwa sasa nipo nje ya Jiji la Dodoma,lakini nitawaagiza maafisa afya na mgambo wa Jiji kufika na kuwachukulia hatua wafanyabiashara hao ambao wameleta sintofahamu ya kukaidi maagizo yaliyotolewa ya kuwazuia wasifanye biashara kwa kuzitandaza chini bali wanatakiwa kutengeneza vichanja,” alisema Mahia.
Leave a comment