MAMA Samia Hassani Suluhu, Makamu wa Rais wa Jamhuri, aweza kuapishwa muda wowote kutoka sasa, kushika madaraka ya rais. Anaripoti Yusuph Katimba, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania, Makamu wa rais, ndiye sasa atakayeapishwa kuchukua nafasi ya Dk. Magufuli, huku Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambacho anatoka rais, kikipewa nafasi ya kuteuwa mtu mwingine wa kushika nafasi ya makamu wa rais.
Hata hivyo, makamu huyo wa rais, atapaswa kutoka Tanzania Bara, kwa kuwa Rais wa Jamhuri, sasa anatokea Zanzibar.
Aidha, kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Jamhuri, ni sharti makamu huyo wa rais atakayependekezwa na rais, baada ya kushauriana na chama chake, atahitaji kuidhinishwa na Bunge.
Katiba inaeleza kuwa rais au makamo wa rais anapofariki dunia; na au kushindwa majukumu yake kwa sababu mbalimbali, hakutakuwa na uchaguzi mwingine, hadi kumalizika kipindi cha miaka mitano cha uongozi wao.
Ibara ya 37 (5) ya Katiba ya Jamhuri inasema, “endapo kiti cha urais kitakuwa wazi kutokana na Rais kufariki dunia, kujiuzulu, kupoteza sifa za uchaguzi au kutumudu kazi zake kutokana na maradhi ya mwili au kushindwa kutekeleza kazi na shughuli za Rais, basi Makamu wa Rais ataapishwa na atakuwa rais wa muda uliobaki katika kipindi cha miaka mitano na kwa masharti yaliyowekwa katika Ibara ya 40.
“Kisha baada ya kushauriana na chama cha siasa anachotoka Rais, atapendekeza jina la mtu atakayekuwa Makamu wa Rais na uteuzi huo utathibitishwa na Bunge kwa kura zisizopungua asimilia hamsini ya wabunge wote.”
Aidha, ibara ya 40 (4) ya Katiba inaeleza, endapo makamu wa Rais anashika kiti cha rais kwa mujibu wa masharti ya Ibara ya 37 (5), kwa kipindi kinachopungua miaka mitatu, ataruhusiwa kugombea nafasi ya rais mara mbili.
“Lakini kama akishika kiti cha rais kwa muda wa miaka mitatu au zaidi, ataruhusiwa kugombea nafasi ya rais mara moja tu.”
Leave a comment