UIMARA wa Chama cha Demokrasia (Chadema), ulioonekana kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, umechangiwa na Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam (endelea).
Dk. Bashiru Ally na Dk. Kitila Mkumbo, Katibu Mkuu Wizara ya Maji na Umwagiliaji, ni miongoni mwa walioshiriki kuandika Sera ya ‘Chadema ni Msingi’ ambayo ilianza kutekelezwa taratibu ambapo sasa imeshika kasi.
Anthony Komu, aliyekuwa Mkurugenzi wa Fedha na Utawala wa Chadema, ametoa historia ya kuanza kwa ‘Chadema ni Msingi’ leo tarehe 19 Februari 2020, wakati akizungumza na viongozi wa Chama cha NCCR-Mageuzi, katika Mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho.
Kwenye historia hiyo, Dk. Kitila na Dk. Bashiru wanaonekana vinara baada ya kuajiriwa na Chadema kuandika sera hiyo. Kabla ya kuajiriwa kwao kuisimamia, ilianza kuandaliwa na wanachama wa Chadema akiwemo Halima Mdee, Mbunge wa Kawe; Yusuph Hamad na Zitto Kabwe ambaye sasa ni Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo.
Komu amesema, sera ya ‘Chadema ni Msingi’ ni zao la ziara ya chama hicho nchini Ghana, ambapo walikwenda kujifunza namna siasa za nchi hiyo zinavyoendeshwa.
“Leo sisi ‘Chadema ni Msingi,’ tunaizungumza ni wazo tulichukua Ghana tukalileta, alikuwepo Zitto, Halima Mdee na Yusuph Hamad. Hawa ndio watu tuliokwenda Ghana, tulipelekwa na chama tukajifunza jinsi inavyofanya kazi na kushinda,” amesema Komu na kuongeza:
“Tukaja kuiandika ‘Chadema ni Msingi’, tukaiandika ile dhana na matamanio yetu, tukawaajiri Kitila Mkumbo na Bashiru Ally ambaye ni Katibu Mkuu CCM, sasa hivi wakaiandika kitalamu. Kamuulizeni Bashiru, waliandika ile ‘Chadema ni Msingi’ ambayo sasa hivi inaendelea kuboreshwa.”
Leave a comment