VIFAA mbalimbali kwa ajili ya kufanikisha uchaguzi mkuu nchini Kenya vimeanza kuwasili nchini humo kutokea Dubai, anaandika Catherine Kayombo.
Miongoni mwa vifaa hivyo ni pamoja na kadi za kupigia kura katika uchaguzi unaotarajia kufanyika Agost 8 mwaka huu.
Tume ya uchaguzi nchini humo imesema kuwa tayari karatasi kwa ajili ya nafasi 47 za magavana 47 zimekuwa za kwanza kuwasili, huku zingine zikitarajiwa kuwasili mwanzoni mwa mwezi ujao.
Hata hivyo, karatasi kwa ajili ya kupigia kura ngazi ya urais hazijaanza kuchapishwa kufuatia mahakama kuu nchini humo kusitisha zabuni ya uchapishaji wake.
Mahakama imedai kuwa karatasi hizo zimesitishwa kutokana na kuhisiwa kwamba kunaweza kutokea dalili za uchochezi na wizi wa kura endapo zitachapisha mapema.
Wananchi na wadau wa uchaguzi wakiwemo wanasiasa wa upinzani wameendelea kuishinikiza tume ya uchaguzi nchini humo kuhakikisha kuwa mashine za kutambua wapiga kura zinafanya kazi ipasavyo.
Wadau hao wameitaka tume kuhakikisha mashine hizo zinafanya kazi vinginevyo upigaji kura uahirishwe katika maeneo ambayo kutakuwa na utata.
Rais Uhuru Kenyata amedai kuwa hizi ni mbinu za upinzani kutaka kuchelewesha uchaguzi.
Naye mgombea urais kupitia chama cha upinzani cha NASA, Raila Odinga amesema kuwa hakuna anayeweza kuzuia vyombo vya habari kujumlisha matokeo kutoka majimboni baada ya mahakama kuruhusu hivyo.
Zikiwa zimesalia siku 20 kuelekea uchaguzi mkuu nchini humo, mvutano wa kisiasa umekua mkubwa hasa kwa chama cha upinzani cha NASA kufuatia kutohudhuria kwenye mdahalo uliondaliwa kwa ajili ya wagombea wote kwa ngazi ya urais.
Leave a comment