JOHN Heche, Waziri Kivuli wa Wizara ya Madini, ameitaka serikali ieleze zilipo fedha kiasi cha Sh. 426 trilioni, zilizokwepwa kulipwa na kampuni ya madini ya Accacia. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Amesema, Rais John Magufuli licha ya kusaini mikataba tisa na kampuni ya madani ya Barick, bado hajaeleza Watanzania kama Accacia ililipa fedha hizo kabla ya kuvunjwa kwake.
Ijumaa tarehe 24 Januari 2020, Rais Magufuli alisaini mikataba na kampuni ya Barrick Gold, makubaliano kati ya kampuni na serikali yalifanyika Ikulu, Dar es Salaam.
Hatua hiyo, ni matokeo ya kutatuliwa kwa mgogoro ulioibuka mwaka 2017 kati ya serikali na kampuni hiyo, na baadaye kuzaliwa kampuni ya Twiga itakayosimamia migodi mitatu iliyokuwa chini ya kampuni ya Acacia (imevunjwa) ambayo ilikuwa mali ya Barick.
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 29 Januari 2020, jijini Dodoma, Heche ameitaka serikali ieleze iwapo fedha hizo zilizokuwa zikikwepwa kulipwa na kampuni ya uchimbaji madini ya Accacia kwa kipindi walichokuwa wakisafirisha makinikia, kama zimelipwa.
Amesema, fedha hizo ambazo zilifanyiwa tathimini na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), zilizoonekana kutolipwa na kampuni hiyo ni Sh. 426 tilioni.
“Juzi wakati mheshimiwa rais anasaini mikataba, hatukusikia popote kinazungumzwa pesa zetu tilioni 426 ambazo zilionekana zimekwepwa na kampuni ya Accacia, kwa kipindi chote ambacho walikuwa wakisafirisha makinikia…
“Juzi walipozungumzia mikataba hii, hawajatuambia Sh. tilioni 426 zilipo, nataka serikali ituambie wamemsamehe mzungu au beberu fedha zetu?” amehoji Heche.
Heche ambaye ni Mbunge wa Tarime vijijini (Chadema), amehoji kwamba iwapo serikali ilimsamehe kiasi hicho cha fedha, je ilitumia sheria gani?
Amesema, iwapo maswali hayo hayatapatiwa majibu, kamati ya Prof. Paramagamba Kabudi, Waziri wa Mambo ya Nje itakuwa imevunja Sheria ya TRA.
Heche amesema, Raia Magufuli alieleza kwamba mteja wa mchanga wa makinikia atafutwe, amehoji je, mteja huyo alipatikana?
“Nahoji kwa kuwa, sheria ya nchi kifungu cha tisa, sheria mpya imekataza kusafirisha mchanga nje ya nchi mpaka ifanyiwa mchakato ikiwa ndani ya nchi,” amesema.
Leave a comment