LIVINGSTON Silinde, Mbunge wa Mvumi (CCM), ameeleza kukerwa na watu wanaomsema vibaya Hayati John Magufuli. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Amesema, anashangazwa na ukimya wa watu waliotetewa na Rais Magufuli wakati wa uhai wake, na kwamba anashambuliwa hata 40 yake haijafika.
Silinde ametoa kauli hiyo leo tarehe 13 Aprili 2021, wakati akichangia Mapato na Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka 2021/2022.
“Leo Magufuli (Hayati Magufuli) anasemwe vibaya na sisi tupo hata 40 haijafika, hili jambo halikubaliki, hawa watu washike adabu na adabu ziwashike. Hatutaki warudie tena mambo ya kipuuzi kama hayo.
“Haiwezekani, hatuwezi kuwavumilia hawa wanaomsema vibaya Magufuli maana watamsema vibaya Samia (Rais Samia Suluhu Hassan), hii ni tabia.

“Hivi leo ni mbunge gani hakutetewa na Magufuli, tupo humu ndani kwa sababu ya Magufuli na Samia (Rais Samia). Walipita kila sehemu kuwaombea kura,” amesema Silinde.
Mbunge huyo amesema, Hayati Magufuli ameifanyia kazi nzuri Tanzania na kwamba, hapaswi kubezwa.
“Lazima tukubaliane, unajua kuna wengine wanafikiri Rais Samia alikuwa nje ya benchi akaingia kucheza mpira hapana, Samia (Rais) alikuwa akicheza pamoja na Magufuli (Hayati Magufuli),” amesema.
Mbunge huyo amesema, haiwezekani kuwa na amani na utulivu wakati kuna watu wanamsema vibaya Hayati Magufuli.
Rais Magufuli aliyefariki dunia tarehe 17 Machi 2021, kwa maradhi ya mfumo wa umeme wa moyo katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho, Dar es Salaam.
Silinde kwa nini asimtaje Spika Ndugai ambaye mara moja amemgeuka JPM na kuanza kuutetea mradi wa Bagamoyo? Msiwe wanafiki