MARA baada ya kuchukua nafasi ya Sven Vandebroeck tarehe 24, Januari 2021, na kuanza kazi ya kukikonoa kikosi cha Simba katika kipindi cha miezi 10 aliyodumu klabuni hapo, Didier Gomes amekuwa moja ya kocha mwenye rekodi nzuri katika michezo mbalimbali ya kimashindano. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Katika michezo yote ya kimashindano, toka alipochukua timu hiyo ikiwa katikati ya msimu, Gomes amefanikiwa kuingoza Simba kwenye michezo 33, ikijumuisha michezo ya Ligi Kuu, kombe la Shirikisho la Azam na michuano ya Ligi ya Mabingwa.
Kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara, Gomes amekiongoza kikosi cha Simba kwenye michezo 19, na kufanikiwa kuibuka na ushindi mechi 15, akisuluhu tatu na kupoteza mmoja.
Kwa upande wa kombe la Shirikisho la Azam, Gomes alikaa kwenye benchi michezo minne na kufanikiwa kushinda yote bila kupoteza hata mmoja.
Aidha kwenye Ligi ya mabingwa barani Afrika, klabu ya Simba chini ya Didier Gomes, imecheza jumla ya michezo 10, ikafanikiwa kushinda 6, kwenda sare mechi moja na kupoteza michezo mitatu.
Mafanikio ya juu katika kipindi cha miezi 10 ya kocha huyo aliyoka ndani ya klabu ya Simba, alifanikiwa kutwaa mataji mawili moja likiwa la Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu wa 2020/21 na kombe la Shirikisho.
Kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, kocha huyo alifanikiwa kuivusha timu hiyo kwenye hatua ya robo fainali, huku akiongoza kundi mbele ya vigogo Al Ahly na As Vita.
Leave a comment