RAIS John Magufuli amesema, Jonathan Shana ambaye ni Kamanda wa Polisi Arusha na Frida Wikesi, Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani humo, ilikuwa awatimue kazi leo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
“Kamanda wa Polisi Arusha na Mkuu wa Takukuru Arusha nilikuwa niwatoe leo, ila nimewasamehe, Sijawasamehe moja kwa moja, najua salamu zitafika. Waambie wakafanye kazi nilizowatuma. Wasimamie sheria sio wafanye kazi zao,” amesema.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Juni 2020, wakati akiwaapisha viongozi wapya – Iddi Kimanta (Mkuu wa Mkoa wa Arusha), Kena Kihongosi (Mkuu wa Wilaya ya Arusha) na Dk. John Pima (Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha), Ikulu jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo amesema, ameamua kuwasamehe kwa sharti la kutorudia tena makosa yao, na kwamba hatosita kuwafuta kazi kama hawatabadilisha mienendo yao.
“Na leo ilikuwa niwatoe RPC pamoja na mkuu wa TAKUKURU Arusha lakini nimeona niwaonye hapahapa, nimeamua kuwasamehe lakini sio moja kwa moja, wakifanya kosa lolote wataondoka. Nataka wakafanye kazi nilizowatuma sio wanazojituma wao,” amesema Rais Magufuli.
Kiongozi huyo wa nchi amemtuma Iddi kuwafikishia salamu Kamanda Shana na Wikesi, kwamba wanatakiwa kufanya kazi alizowatuma na si kufanya kazi wanazojituma wenyewe.
“Najua mtawafikishia salamu, nimejitahidi sana kuwasamehe, haiwezekani mmetwauma kazi za serikali wanafanya za kwao, RC Arusha kawafikishie ujumbe wafanye kazi walizotumwa kulingana na mamlaka yao, wasimamie sheria na maadili yao,” amesema Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli amewataka watendaji wa Halmashauri ya Jiji la Arusha, kufanya kazi zao kwa mujibu wa sheria.
Leave a comment