MBUNGE wa Jimbo la Mtwara Vijijini Hawa Ghasia (CCM) amejikuta katika wakati mgumu baada ya mezomewa na baadhi ya wabunge pamoja na wadau mbalimbali wa elimu baada ya kutoa kauli ya kejeri kwa walimu, anaandika Dany Tibason.
Ghasia alizomewa wakati wa kuchangia mjadala wa uzinduzi wa ripoti ya uwezo, utafiti wa kitaifa unaopima kujifunza kwa watoto ambapo umefanyika katika ukumbi wa Hazina mjini Dodoma.
Wabunge na wadau wamelazimika kumzomea Ghasia baada ya kutoa kauli za kuwakejeri walimu kwa kusema kuwa walimu ni watu wanaopenda kulalamika.
Mbali ya kudai kuwa walimu ni kati ya kada ambayo inapenda kulalamika pia amesema walimu wanalipwa vizuri tofauti na watumishi wengine huku akidai kuwa wanaolipwa vizuri ni madaktari.
Lengo la uzinduzi huo ni kujadili mambo 10 muhimu kuhusu elimu ya Tanzania.
Mambo hayo yalitajwa kuwa ni ujuzi wa kusoma na kuhesabu bado upo chini kwa wanafunzi wa shule za msingi na haujafikia kiwango kinachotakiwa katika mitaalam.
Pia ripoti hiyo ilieleza kuwa kwa ujumla hakuna mabadiliko makubwa kwenye matokeo ya kujifunza kati ya mwaka 2011 na mwaka 2015.
Viwango vya ufaulu wa somo la kiswahili vimeongezeka sana na bado vinazidi vile vya somo la kiingereza. Hata hivyo, viwango vya ufaulu katika somo la hisabati havijabadilika ndani ya kipindi cha miaka mitatu.
Akina mama wenye elimu ya sekondari na kuendelea wanaonekana kuwa na watoto wanaofaulu zaidi kuliko akina mama ambao hawajasoma.
Akiendelea kutoa taarifa ya ripoti hiyo ilionesha kuwa matokeo ya kujifunza yanatofautiana sana katika ngazi ya mkoa wa wilaya.
Katika hatua nyingine alielezwa kuwa viwango vya uandikishwaji wa wanafunzi shuleni vimeendelea kuwa juu. Hata hivyo viwango hivi vimeshuka kidogo ndani ya miaka ya hivi karibuni hasa katika maeneo ya vijijini.
Akisoma taarifa hiyo Zaida Mgalla ambaye ni Meneja uwezo Twaweza amesema asilimia ya watoto ambao wanasoma darasa lisiloendana na umri wao umezidi kuongezeka.
Katika ripoti hiyo 8 kitaifa upatikanaji wa vitabu umeongezeka hasa kwa madarasa ya chini kiswahili, kingereza na hisabati.
Aidha amesema viwango vya watoto wa walimu na wanafunzi bado viko juu na shule chache hutoa huduma ya chakula japokuwa kutokufanya hivyo kuna athiri hali ya lishe na uwezo wake wa kujifunza.
Naye Suzana Lyimo na Mbunge wa Iringa Mjini Mchungaji Peter Msigwa, wamesema serikali bado haijaelekeza nguvu katika kutatua changamoto mbalimbali amazo zinawakabili walimu.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Tamisemi, Selemani Jafo amesema taarifa ya Twaweza itafanyiwa kazi ambazo zimeweza kuibuliwa na utafiti huo.
Leave a comment