MAHAKAMA Kuu, Kanda ya Dar es Salaam, inatarajia kutoa hukumu ya uamuzi wa rufaa ya mwenyekiti wa taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe na mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mbowe na Matiko, waliwasilisha rufaa hiyo mahakama kuu, kupinga uamuzi wa mahakama ya Hakimu Mkuu Mkazi Kisutu, kufuatia mahakama hiyo kudai washitakiwa hao walikiuka dhamana.
Hukumu hiyo itatolewa kesho saa 7 mchana, mbele ya Jaji Sam Rumanyika.
Dhamana ya Mbowe na Matiko ilifutwa na Wilbard Mashauri aliyekuwa Hakimu Mkazi kwenye mahakama hiyo. Kwa sasa, Mashauri ni jaji wa mahakama kuu. Wanasiasa hao wawili, walifutiwa dhamana tarehe 30 Novemba mwaka jana.
Kupitia mawakili wao, Peter Kibatara na Jerimiah Mtobyesya, walieleza mahakama kuu kuwa uamuzi wa hakimu Mashauri ufutwe kwa sababu hakujielekeza kwa wadhamini wa Mbowe na Matiko waliosaini dhamana kwa ajili ya kuwadhamini watuhumiwa.
Upande wa Jamhuri uliowakiliswa na mawakili waandamizi Simon Wankyo, Faraja Nchimbi na Paul Kadushi.
Kibatara amesema, uamuzi wa Mahakama ya Kisutu haukuwa sahihi na ulitolewa kinyume na sheria.
“Hoja kuwa Mahakama ijielejeze kwa wadhamini, ni dhaifu mno na kinyume na sheria,” ameeleza.
Hata hivyo, upande wa mashitaka umepinga maelezo hayo kwa madai kuwa warufani hao walikiuka masharti ya dhamana na kwamba hawakuwepo mahakamani.
Baada ya kusikiliza hoja za pande zote jaji Rumanyika aliahilisha shauli hilo na kuliita kesho kwa ajili ya hukumu.
Kesi ya msingi, Mbowe, Matiko na watu wengine saba, wanakabiliwa na mashitaka 13, ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko wenye ghasia, kuhamasisha hisia za chuki, kushawishi hali ya kutoridhika, uchochezi na kushawishi utendaji wa kosa la jinai. Wanadaiwa kutenda kosa hilo, kati ya 1 Februari na 16 Machi, mwaka jana, maeneo ya Dar es Salaam.
Washitakiwa wengine kwenye kesi hiyo, ni Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Vincent Mashinji; Mbunge wa Iriga Mjini, Mchungaji Peter Msigwa na Mbunge wa Kibamba na Katibu wa Chadema, Tanzania Bara, John Mnyika.
Wengine, ni Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya, Mbunge wa Kawe na Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la chama hicho (BAWACHA), Halima Mdee; Mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche na Naibu Katibu Mkuu (Zanzibar), Salum Mwalimu.
Leave a comment