MAHAKAMA Kuu kanda ya Dar es Salaam, itatoa maamuzi ya kesi ndogo ya zuio la uchaguzi namba 305, iliyofunguliwa na mwanamichezo Ally Saleh ‘Alberto’ tarehe 16 Julai, 2021, baada ya pande zote mbili kukamilisha kuwasilisha hoja zao. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Shauri hilo dogo ambalo limesikilizwa kwa wiki nzima kuanzia tarehe 2-9 Julai 2021, chini ya Jaji Edwin Kakolaki, kabla ya kesi ya msingi namba 98/2021 kusikilizwa, ambapo upande wa Ally Salehe uliwakilishwa na Mawakili, Frank Chacha pamoja na Jeremieh Mtobesya.
Katika shauri hilo, wakili anayesimama upande wa TFF, Bodi ya wadhamini na Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, John Mshumbuzi alitoa pendekezo la mahakama hiyo kutoweka zuio hilo kwenye uchaguzi Mkuu wa Shirikisho hilo kwa wao ni wanachama wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Dunia (FIFA).
Mshumbuzi aliwasilisha hoja hiyo kuwa endapo zuio hilo litawekwa, basi FIFA inaweza kuchukua hatua kwa Tanzania kama kufungia timu zake kushiriki michuano mbalimbali ya kimataifa ikiwemo kwa klabu zake za Simba na Yanga.
Jaji Kakolaki alisema kuwa kwa sasa kinachodaiwa kwenye shauri hilo ni suala la uchaguzi wa TFF, na kuuliza kwani bila klabu hizo mbili mambo hayatoenda? Licha ya kuichukua hoja hiyo.
Wakili wa upande wa wadai, Frank Chacha alizungumza baada ya kuhailishwa kwa kesi hiyo na kufunguka kwamba lengo lao kuu kwenye shauri hilo dogo ni kutaka shughuli zote za uchaguzi zisimamishwe.
“Tunaomba shughuli zote za uchaguzi zisimame mpaka kesi yetu ya msingi namba 98 ya mwaka 2021, itakaposikilizwa,” alisema Wakili Chacha.
Mara baada ya mawasilisho ya hoja za pande zote mbili kwenye mahakama hiyo, Jaji Kakolaki alisema kuwa hukumu ndogo juu ya shauri hilo, itatolewa siku ya Ijumaa ya tarehe 16 Julai 2021, sambamba na kuanza kusikiliza kesi ya msingi.
Uchaguzi huo umepangwa kufanyika tarehe 8 Agosti, 2021, jijini Tanga, ambapo mpaka sasa kamati ya uchaguzi imempitisha Wallace Karia kuwa mgombea pekee kwenye nafasi ya Urais. Karia ni rais wa shirikisho hilo kwa sasa.
Ally Saleh ambaye pia ni wakala anayetambulika na Shirikisho la Mpira wa Miguu, Barani Afrika (CAF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Dunia (FIFA)alifungua kesi hiyo tarehe 1 julai 2021, kwenye Mahakama Kuu, mara baada ya kuenguliwa kwenye kinyang’anyiro hiko kutokana na kukosa wadhamini watano ambao ni vyma vya mikoa na klabu za mpira kutoka Tanzania Bara.
Juni 14 Mwaka huu, Ally Salehe aliiibua na malalamiko yake kuhusu kinachoendelea kwenye uchaguzi huo, huku akiibua hoja ya ushiriki wa Zanzibar kwenye uchaguzi huo na kusema kuwa kuja haja ya kuangalia muundo wa Shirikisho hilo, kwa kuwa ushiriki wa Zanzibar ni finyu.
Leave a comment