MAMA yangu aliniambia, Mungu alimuepusha uchungu mkali wakati wa kunizaa lakini sasa anapata machungu makali kila siku katika utu uzima wangu. Anaandika Hamis Mguta…(endelea).
Ni kauli ya Halima Mdee, Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) – Taifa (BAWACHA), aliyoitoa tarehe 4 Agosti 2019 wakati akihutubia baraza hilo kwenye ufunguzi wa kongamano la wanawake.
Kongamano hilo lilifanyika katika ofisi kuu za chama zilizopo Mtaa wa Ufipa, Kinondoni, Dar es Salaam.
“Mama yangu aliwahi kuniambia ‘mwanangu, sikujua kuwa Mungu aliniepusha na uchungu wakati nakuzaa lakini nakutana na uchungu kilasiku ya utu uzima wako’.
“… hiyo ndio kauli ya Mama yangu, namuonea huruma kwasababu kila shida ninayopata mimi, nachukulia poa sana lakini mama yangu anakuwa kwenye mateso makubwa,” amesema.
Kwenye kongamano hilo Mdee amesema, katika awamu zote za uongozi chini ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), awamu ngumu kuliko zote ni awamu ya sasa.
“Hii ndio awamu ngumu kupita kipindi chote. Watu wanapitia misukosuko mikubwa na yenye kukatisha tamaa lakini tupambane,” amesema na kuongeza:
“Katika kipindi hiki, wanawake wametwezeka na kauli za kebehi dhidi yao huku kauli za wakubwa zinatafsiri wazi kuwa ni kama vyombo vya starehe na sio watu.”
Amesema, kuna maeneo mengi ambayo mtoto wa kike akiwa kwenye hedhi, lakini kwa kukosa kifaa cha kumuhifadhi (taulo), kunasababisha akose kufika shule kwa siku tano mpaka saba anakaa nyumbani ili kadhia iishe arudi shule.
“…serikali inaambiwa Kenya na Uganda wametoa msamaha kwa taulo za kike ili kunyanyua ufaulu wa wanawake, bado serikali hii ya wanyonge inakataa, nenda google angalia kauli za kebehi dhidi ya wanawake, Tanzania hakuna kipindi ambacho tumetwezeka kama kipindi hiki,”amesema.
Leave a comment