MBUNGE wa Kawe Halima Mdee (Chadema) ameitaka serikali ieleze ni lini sheria kandamizi kwa akina mama zitaondolewa hasa katika upande wa umilikaji na umilikishwaji wa hardhi, anaandika Dany Tibason.
Mdee alitoa kauli hiyo leo bungeni alipouliza swali la nyongeza akieleza kuwa asilimia ya 70 ya wazalishaji ni wanawake 70% lakini wanaomiliki ardhi ni 20% Je, serikali haioni kama sheria ya ardhi ni kandamizi kwa wanawake ambao ni wazalishaji zaidi.
Aidha katika swali lake la nyongeza mbunge huyo amesema,sheria ya umilikaji wa ardhi kwa sasa ni kandamizi na wapo wanawake wanaomiliki ardhi lakini wanashindwa kupatiwa hati jambo ambalo linasababisha kushindwa kupata mikopo katika taasisi za kibenki.
Awali katika wali la msingi la mbunge wa viti maalum, Bupe Mwakang’ata (CCM) alitaka kujua Serikali inawasaidiaje wananchi na hasa wanawake kwa kuzungumza na benki zikubali kupokea hati za kimila kama dhamana ya mikopo.
“Lengo la serikali ni kuwainua kiuchumi wananchi maskini vijijini hasa wanawake ambao hawana dhamana ya kuweka benki ili waweze kupata mikopo kwa sababu nyumba nyingi za vijijini hazina hati miliki kama dhamana ya benki.
“Je, Serikali Serikali inawasaidiaje wananchi na hasa wanawake kwa kuzungumza na benki zikubali kupokea hati za kimila kama dhamana ya mikopo,” amehoji Mwakang’ata.
Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kawe, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi amesema kwa sasa hakuna mwanamke ambaye anaweza kupoteza haki yake ya kumiliki ardhi.
Amesema kwa sasa hati ubadilishwa majina au mtu anapotaka kuuza sehemu yake ni lazima wahusishwe watu wote kwa maana ya mwanamke na mwanaume.
“Kwa sasa tunafanya utaratibu ambao utamfanya kila mmoja kuhakikisha kinachofanyika kuhusu kubadilisha hati au kuuza wahusika wote ni lazima wahusike.
“Kama hati ni ya mama anataka kuuza ni lazima mwanaume ahusishwe na kama hati ni ya mwanaume ni lazima mwanamke hausishwe kwa sasa hakuna mtu ambaye naweza kubadilisha hati peke yake bila kuhusisha pande zote mbili ili asiwepo mtu wa kupoteza,” ameeleza Lukuvi.
Naye Naibu wa Wizara hiyo, Angellina Mabula akijibu swali la msingi amesema utoaji wa hati za kimila ni sehemu ya utekelezaji wa sheria ya ardhi ya vijiji Na.5 ya mwaka 1999 na kanuni zake.
Leave a comment