MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi mkoa wa Iringa imekataa ombi la Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo la kukataa kuendelea usikilizwaji wa kesi yake mbele ya Hakimu John Mpitanjia. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Nondo anayeshtakiwa mahakamani hapo kwa tuhuma za kudaiwa kujiteka na kusambaza taarifa za uongo katika mitandao ya kijamii, alimkataa Hakimu Mpitanjia kwa madai ya kutokuwa na imani naye.
Hakimu Mpitanjia amegoma kujitoa katika kesi hiyo kutokana na sababu za kumkataa ni za kufikirika na hazina mashiko.
Nondo aliwasilisha maombi ya kumkataa Hakimu huyo juzi kwa njia ya barua kwa kile alichoeleza kuwa hana imani na hakimu huyo ikiwa pamoja na sababu ya ukaribu wa hakimu huyo na Mkuu wa upelelezi wa jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa.
Akitoa uamuzi huo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa, Hakimu Mpitanjia amesema sababu alizotoa mshtakiwa hazina msingi wowote na ataendelea kusikiliza shauri hilo kwani akijitoa haki itachelewa.
“Sababu walizotoa upande wa utetezi ni za kufikirika ambazo hazina ushahidi wowote na kwa kuwa mahakama ni chombo cha mwisho katika kutenda haki na kuwahisha haki, nitaendelea kusikiliza shauri hili ili niwahishe haki ya mshtakiwa kwa mujibu wa sheria,” amesema Hakimu Mpitanjia.
Jebra Kambole, wakili wa Nondo akizungumzia uamuzi huo amesema upande wa utetezi wamepokea uamuzi wa mahakama na hawawezi kuupinga ila kama kutakuwa kuna ulazima wa kufanya jambo lolote la kisheria watatumia njia nyingine za kupata haki yao.
“Kwa sasa tunaona shauri liendelee tu ili mshtakiwa aendelee na mambo mengine, kama anafungwa afungwe na kama anaachiwa aachiwe akaendelee na shule,” amesema Kambole.
Leave a comment