MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imehairisha kesi namba 75 ya mwaka 2019 inayomkabili mwandishi wa kujitegemea wa habari za uchunguzi nchini, Erick Kabendera kutokana na upande wa Serikali kushindwa kukamilisha upelelezi. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mbele ya Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo Augustina Mmbando, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon ameiomba mahakama hiyo kuahirisha shauri hilo kwa madai kuwa hakimu anayesikiliza shauri hilo Augustine Rwizile amepata dharura pia upande wao haujakamilisha upelelezi wa shauri hilo.
Jebra Kambole ambaye ni Wakili anayeongoza jopo la utetezi ameiomba mahakama hiyo kuwa upande wa Serikali uharakishe upelelezi kutokana na mshtakiwa kuwa hana dhamana.
Nje ya Mahakama hiyo, Mratibu wa Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo Olengurumwa amesema kuwa mashtaka yanayomkabili Kabendera yametokana na kazi zake anazozifanya, hivyo wadau wote wa habari na haki za binadamu nchini na ulimwenguni kwa ujumla wanapaswa kupaza sauti zao ili haki itendeke dhidi ya mwandishi huyo.
Aidha Olengurumwa ameviomba vyombo vinavyosimamia utoaji haki nchini ikiwemo vyombo vya uchunguzi kuchunguza kwanza kabla mshtakiwa hajafikishwa mahakamani ili kuepuka wimbi la mrundikano wa kesi nyingi mahakamani kutokana na uchunguzi kutokukamilika.
Kesi hiyo imeahirishwa mpaka Agosti 30, 2019.
Leave a comment