WAZIRI wa Nishati, Januari Makamba, amesema Serikali ina mpango wa kufumua gridi ya taifa, ili kuboresha miundombinu yake chakavu inayosababisha changamoto ya kukatika kwa umeme nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni jijini Dodoma, leo tarehe 3 Februari 2023, Makamba amesema kuwa, tarehe 15 Februari mwaka huu, Serikali itasaini mkataba wa mradi wa kuboresha gridi hiyo “Gridi Imara” wenye thamani yaSh. 1 trilioni, ili kuimarisha usambazaji wa umeme.
“Kuhusu umeme kukatika tunafahamu changamoto bado ipo, lakini ninachotaka kuwahakikishia Watanzania hivi tunavyoongea tunayo mipango madhubuti ya kuifumua gridi nzima na kuirekebisha sababu changamoto kubwa iliyokuwepo ni miundombinu chakavu. Miundombinu yetu ya usafirishaji na usambazaji umeme ilikuwa haitoshelezi mahitaji na ilikuwa haijafanyiwa marekebisho muda mrefu,” amesema Makamba.
Katika hatua nyingine, Makamba amesema Serikali imeweka taratibu mpya za kutafuta wakandarasi wa ujenzi wa miradi ya umeme ikiwemo katika Wakala wa Nishati Vijijini (REA), ambapo miongoni mwa vigezo hivyo ni kutowapa tenda wakandarasi wenye malimbikizo ya miradi.
“Baada ya kubaini changamoto zilizopo tumebadilisha utaratibu wa manunuzi, usimamiajia na tathimini ya miradi hii. Mfano utaratibu wa vigezo vya mkandarasi kupata mradi vitakuwa tofauti kwamba hawezi kupata mradi mpaka alio nao awe amefikia asilimia 60. Kutakuwa na kundi la wakandarasi mahiri ambao watakuwa wamepitia vigezo, atakayemaliza haraka ndiyo atapata kazi nyingine,” amesema Makamba.
Katika hatua nyingine, Makamba amesema Serikali imeajiri watumishi 136 kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wa miradi ya REA majimboni ambao watakuwa wanatoa ripoti serikalini kuhusu hatua zinazofikiwa.
Leave a comment