MAHAKAMA ya Milimani nchini Kenya, imemuacha kwa dhamana ya Ksh. 15 milioni, Mike Sonko, Gavana wa Nairobi anayekabiliwa na mashataka ya ufisadi. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Uamuzi wa dhamana hiyo umetolewa leo tarehe 11 Desemba 2019, na Douglas Ogoti, Hakimu Mkuu wa Mahakama hiyo, kitengo cha ufisadi.
Dhamana hiyo imetolewa siku tano, baada ya Sonko kuwekwa kizuizini na polisi, tangu alipokamatwa Ijumaa ya tarehe 6 Desemba 2019.
Aidha, mahakama hiyo imempiga marufuku Gavana Sonk kufika katika ofisi yake, hadi pale kesi yake itakapotolewa uamuzi.
Hata hivyo, Hakimu Ogoti amesema kama kutakuwa na uhitaji wa gavana huyo kufika ofisini kwake, atasindikizwa na maafisa wa uchunguzi.
Vile vile, Gavana Sonko ameamriwa kupeleka hati zake za kusafiria (Passport) pamoja na nyaraka nyingine za usafiri, mahakamani hapo.
Baada ya uamuzi huo, Hakimu Ogoti amesema kesi hiyo itatajwa tarehe 15 Januari 2020.
Gavana Sonko amefunguliwa mashtaka zaidi ya 30 mahakamani hapo, miongoni mwa mashtaka hayo ni utakatishaji fedha, kupokea rushwa pamoja na kutumia vibaya madaraka kwa maslahi yake binafsi.
Leave a comment