ALIYEWAHI kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndulu (71), amefariki dunia leo Jumatatu tarehe 22 Februari 2021, katika Hospitali ya Kairuki, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Profesa Ndulu, aliyezaliwa tarehe 23 Januari 1950, alikuwa Gavana kwa miaka kumi, kati ya mwaka 2008 hadi 2018.
Aliteuliwa Januari 2008 na Rais wa wakati huo, Jakaya Kikwete kuwa Gavana, nafasi aliyohudumu hadi Januari 2018, ambapo Rais John Magufuli, alimteua Profesa Florens Luoga kushika nyadhifa hiyo.
Kabla ya uteuzi huo, Profesa Luoga, alikuwa Mhadhiri wa uchumi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), sawa na mtangulizi wake, Profesa Ndulu.
Profesa Ndulu, aliteuliwa kushika wadhifa huo, baada ya aliyekuwa gavana, Daudi Balali, kufariki dunia mwaka 2008.
Kifo cha mchumi huyo mbobezi, Profesa Ndulu, kimekuja ikiwa ni takribani siku mbili kupita, tangu mchumi mwingine, Dk. Servacius Likwalile, aliyewahi kuwa katibu mkuu wizara ya fedha na mipango, kufariki dunia.
Dk. Likwalile, alifariki usiku wa kuamkia Jumamosi, tarehe 20 Februari 2021, katika Hospitali ya Regency, Dar es Salaam, baada ya kuugua kwa muda mfupi.
Profesa Ndulu na Dk. Likwalile, walifanya kazi pamoja, mmoja akiwa gavana na mwingine katibu mkuu na wote kwa pamoja, walikuwa wahadhiri waandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Prof. Benno Ndulu, mchumi uliyebobea, mwalimu mwenzetu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, umelitumikia Taifa lako #Tanzania, umeitumikia #Africa na Dunia nzima, kwa weledi wa hali ya juu. Naipa pole familia, Benki Kuu ya Tanzania, na WanaIfakara. Pumzika kwa amani, milele. RIP. pic.twitter.com/CWH2aV4tQz
— Mark J. Mwandosya (@MarkMwandosya) February 22, 2021
Zitto Kabwe, Kiongozi wa ACT-Wazalendo, ameandika katika ukurasa wake wa Twitter “Kwa heri Mzee wangu Prof Benno Ndulu. Sina nguvu za kusema zaidi ya Kwa Heri.”
“Namshukuru Mola kwa kunipa nafasi ya kufanya kazi nawe kwa miaka nane. Namshukuru Mola wetu kuwa tulionana wiki chache kabla ya umauti Wako. Tangulia Prof tangulia Mchumi wetu uliyetukuka,” ameandika
Zitto aliyekuwa mbunge wa Kigoma Kaskazini na baadaye Kigoma Mjini kwa miaka 15, alikuwa mwenyekiti wa kamati ya bunge ya hesabu za serikai, nafasi iliyomwezesha kufanya kazi na BoT, chini ya Profesa Ndulu.
Leave a comment