HALIMA Mdee, mbunge wa Kawe, ameshindwa kufika mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam kusikiliza madai ya kumdhalilisha Rais John Magufuli, baada ya kuharibikiwa na gari. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Fareson Rukomo ambaye ni mdhamini wa Mdee leo tarehe 29 Oktoba 2019, ameieleza mahakama hiyo, kwamba mdhaminiwa wake ameshindwa kuhudhuria kesi yake baada ya kupata tatizo hilo.
Shahidi huyo amesema, alipigiwa simu na Mdee kwamba alikuwa safarini kutoka Dodoma kwenda Dar es Salaam ili kuhudhuria shauri hilo, lakini gari lake limeharibikia kati ya Dodoma na Morogoro.
Mdee anakabiliwa na kesi ya kutoa lugha chafu dhidi ya Rais Magufuli, alipokuwa kwenye mkutano wake uliofanyika Makao Makuu ya Chama cha Demokraia na Maendeleo (Chadema), Kinondoni Dar es Salaam.
Inadaiwa tarehe 3 Julai 2017, Makao Makuu ya Chadema, Mdee alitamka maneno ya kuudhi dhidi ya Rais Magufuli kwamba ‘anaongea hovyo, anatakiwa afungwe breki.’
Hata hivyo, Wakili wa Jamhuri Wankyo Simon, ameieleza mahakama hiyo kwamba shauri limefikishwa hapo kwa ajili ya kusikilizwa.
Mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakili huyo ameeleza, shahidi aliyetegemewa kuendelea na ushahidi kwenye shauri hilo, hakufika.
Hakimu Simba ameahirisha shauri hilo mpaka tarehe 8 Novemba 2019.
Leave a comment